WAKAZI wa Manispaa ya Musoma, mkoani Mara, wameanza kuonja makali ya bajeti ya mwaka 2007/08 baada ya kupanda kwa bei ya dizeli na petroli katika vituo mbalimbali vya mafuta mjini hapa, hivyo kusababisha nauli na bidhaa mbalimbali muhimu kupanda pia.
Uchunguzi uliofanywa na Tanzania Daima jana na juzi, umebaini kuwa bei ya mafuta ya dizeli imepanda kutoka sh 1,200 hadi sh 1,600 kwa lita, ikiwa ni ongezeko la sh 400. Pia bei ya mafuta ya petroli imeongezeka kutoka sh 1,500 hadi sh 1,600 kwa lita, ikiwa ni ongezeko la sh 150.
Bei ya dizeli imeongezeka kwa kiwango kikubwa zaidi ukilinganisha na petroli kwa kuwa vyombo vingi vya usafiri, mashine na mitambo mbalimbali vinatumia aina hiyo ya mafuta.
Kupanda huko kwa bei ya dizeli na petroli kumesababisha kuongezeka kwa nauli za mabasi makubwa na madogo ya abiria yanayoingia na kutoka katika Manispaa ya Musoma.
Kwa sasa nauli ya basi kutoka Musoma kwenda Mwanza imepanda kutoka sh 5,000 hadi sh 6,000, wakati nauli kutoka Mjini hapa kwenda maeneo mbalimbali ya Musoma Vijijini imepanda kutoka sh 2,000 hadi sh 3,000.
Aidha, nauli ya basi kutoka Musoma kwenda Tarime imepanda kutoka sh 2,000 hadi sh 3,500, wakati kutoka Musoma hadi Sirari imepanda kutoka sh 3,000 hadi sh 4,000.
Kutokana na kupanda kwa mafuta kulikosababisha kupanda kwa nauli, baadhi ya wakazi wa mjini hapa wanasema kuwa huu ni mwanzo tu wa maisha kuwa magumu zaidi, kwani wanaamini bidhaa nyingine muhimu kama vile vyakula, sukari, sabuni na vifaa vya ujenzi pia vitapanda bei.
“Huu ni mwanzo wa maisha magumu zaidi kwa mwananchi wa kawaida, kwani tunafahamu wazi kuwa kupanda kwa bei ya mafuta kutapandisha bei ya vitu vyote muhimu. Sijui bajeti hiyo ina manufaa gani kwetu wenye kipato cha chini,” alisema Salome John, mkazi wa Nyasho.
Madereva wa mabasi waliiambia Tanzania Daima kuwa, wamepandisha nauli kutokana na kupanda kwa bei ya mafuta.