SIKU chache baada ya kuripotiwa kutokea wizi katika Wizara ya Miundombinu bila kuvunjwa mlango, wizi mwingine wa aina hiyo umetokea katika Ofisi ya Katibu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Damian Foka.
Habari za kuaminika toka ofisi za Bunge jijini Dar es Salaam, zinaeleza kuwa, watu wasiojulikana, bila ya kuvunja mlango, waliiba kompyuta ya katibu huyo ambayo inatumiwa kwa shughuli za kikazi.
Kwa mujibu wa vyanzo hivyo, kompyuta hiyo iliibwa wakati Foka akiwa kwenye vikao vya Bunge vinavyoendelea mjini Dodoma, na kuongeza kwamba wafanyakazi katika ofisi hiyo walibaini asubuhi kuwa kompyuta hiyo imeibwa.
“Hata sisi tunashangaa kompyuta hii imeibwaje, kwani ni ya mezani na wala mlango wa ofisi ya katibu haujavunjwa na walinzi walikuwepo, lakini eti nao wanasema hawajaona kompyuta hiyo ilivyoibwa,” kilipasha chanzo chetu.
Aidha, vyanzo hivyo vilieleza kwamba, tayari uchunguzi wa siri umeanza, ili kubaini wahusika wa tukio hilo ili waweze kuchukuliwa hatua za kisheria.
“Kwa kweli hata sisi tumekumbwa na wasiwasi ni kwanini wezi wale washindwe kuiba kompyuta za Katibu Muhtasi wake au za ofisi nyingine hadi waibe kompyuta ya Katibu… si siri hali tete imetanda ndani ya ofisi hii kwakuwa wengi wanaamini wizi huu ni njama za baadhi ya watu ambao wanataka kujua siri za Bunge kwani Katibu wa Bunge ndiyo injini ya Bunge,” alisema ofisa mmoja mwandamizi wa Bunge, Dar es Salaam.
Naye Katibu wa Bunge Damian Foka, alipoulizwa kuhusu wizi huo kwa njia ya simu jana, alikiri kupokea taarifa kutoka kwa wasaidizi wake, kwamba kompyuta yake imeibwa na watu wasiofahamika.
“Ndugu mwandishi ni kweli nimepokea taarifa za kuibwa kwa kompyuta ninayoitumia niwapo ofisi za Bunge Dar es Salaam, ila hadi sasa hajakamatwa mtu aliyehusika na tukio hilo,” alisema Foka.
Aidha, baadhi ya wafanyakazi wa ofisi hiyo wameonyesha kukerwa na tukio hilo linalodhalilisha ofisi hiyo kuwa ina ulinzi legelege jambo ambalo ni hatari kwa usalama wa taifa.
“Tunashauri ulinzi uimarishwe ndani ya jengo hili kwani taarifa hizi za kuibwa kwa kompyuta ya katibu zinazua maswali mengi kuliko majibu, lakini binafsi yangu naamini waliohusika na tukio hili ni watu wa humu humu ndani, haiwezekani mtu wa nje atoke huko alikotoka aje kuiba kwenye ofisi kubwa kama hii,” kilisema chanzo chetu