VIONGOZI wanne wa kambi ya upinzani waliozuru Mkoa wa Kigoma, wameutangaza kuwa moja ya ngome kuu za kambi ya upinnzani.
Uamuzi wa kuutangaza mkoa huo kuwa moja ya ngome kuu za kambi ya upinzani umekuja baada ya idadi kubwa ya wanachama wa kambi hiyo waliohamia Chama Cha Mapinduzi (CCM) hivi karibuni kujitokeza na kueleza kuwa hawakukabidhi kadi zao za uanachama walipotangaza kuhama.
Mwenyekiti wa Kitongoji cha Bweni, Kata ya Nguruka, Shukuru Petro (NCCR-Mageuzi) aliwaeleza viongozi wanne hao, Freeman Mbowe (CHADEMA) Prof. Ibrahim Lipumba (CUF), James Mbatia (NCCR - Mageuzi) na Augustine Mrema (TLP), kuwa viongozi wa CCM mkoani Kigoma waliwanunua wanachama hao ili kumfurahisha Rais Kikwete.
Petro alisema habari zilizotangazwa awali kuwa wenyeviti wa Serikali za Mitaa 73 wa vyama vya upinzani wamehamia CCM hazikuwa sahihi, na zilitolewa kwa lengo la kudhoofisha nguvu ya upinzani mkoani humo na nchini kwa ujumla.
Alisema wenyeviti waliotangaza kuhama wakati wa ziara ya Rais Kikwete ni 32, ambao hata hivyo baada ya kukutana na wenyeviti hao wa kambi ya upinzani waliomba radhi na kurejea katika vyama vyao vya awali.
Kurudi kwa wenyeviti hao kumeelezwa na wenyeviti hao kama ushindi mkubwa dhidi ya chama tawala walichokishutumu kuwa kimekuwa kikitumia ushawishi wa fedha kununua wanachama wa vyama vya upinzani ili kumaliza nguvu ya upinzani nchini.
Katika taarifa yake kwa viongozi hao, Katibu wa CHADEMA mkoani hapa, Msafiri Wamalwa, alieleza kuwa wenyeviti hao walirudi na kuomba radhi baada tu ya ziara ya Rais Kikwete kumalizika mkoani humo.
Wamalwa alisema katika maelezo yao, walieleza kuwa walilazimika kukubali kutangaza kuwa wamejiunga na CCM baada ya kupatiwa fedha, hata hivyo baadhi yao walikataa kukabidhi kadi za uanachama wa CHADEMA na kwamba waliopokea kadi za kujiunga na CCM ni wanne tu.
“Walikuja tukazungumza nao baada tu ya Rais Kikwete kuondoka mkoani hapo, wakakiri kuwa walipewa pesa hivyo wakakubali kutangaza kujiunga na CCM, lakini ni wanne tu waliopokea kadi za CCM kwa niaba ya wenzao na wala hawakukabidhi kadi za CHADEMA, baadhi walichokifanya walikabidhi zile za zamani,” alisema Wamalwa.
Alisema kwa sababu wanamageuzi hao hawakukabidhi barua za kujiuzulu wala kufutiwa udhamini na vyama vyao, wanaendelea kuwa viongozi wa upinzani kwa vile kanuni za uchaguzi za serikali za mitaa zinaendelea kuwatambua kama viongozi wa kambi ya upinzani.
Katika mikutano miwili waliyoifanya jana, viongozi hao katika hotuba zao waliikosoa serikali kwa kuutenga Mkoa wa Kigoma kimaendeleo.
Pia walieleza kutoridhishwa kwao na bajeti ya 2007/2008 kuwa haikuwajali wananchi wa chini na mwelekeo wake ni kupanda kwa gharama ya maisha.
Hata hivyo, ziara ya viongozi hao imekuwa nyuma ya wakati kutokana na wananchi wengi kusimamisha msafara wao wakitaka kusikia hotuba zao.
Msafara wa viongozi hao jana ulilazimika kusimama kwa muda mrefu wakati ukitokea Ujiji kuelekea Jimbo la Kigoma Kusini, Kata ya Nguruka, baada ya wananchi kufunga barabara wakiwataka viongozi hao kusimama na kuwahutubia.
Walizuiliwa pia katika Kijiji cha Malagarasi, lakini walifanikiwa kuwahi mkutano uliokuwa umepangwa kufanyika Kata yaNgaruka.
Katika kata hiyo, wenyeviti 42 wa serikali za mitaa kupitia Chama cha NCCR -Mageuzi walilalamika kuwa baadhi ya viongozi wa serikali wamekuwa wakiandika majina yao na kuyapeleka kwa Mkurugenzi wa Manispaa wakidai kuwa wamehama vyao na kujiunga na CCM hivyo kupoteza nafasi zao za uongozi.
Akihutubia katika mkutano huo, Mwenyekiti wa NCCR -Mageuzi, James Mbatia, alisema kambi ya upinzani italishughulikia suala la wanachama hao pamoja na madai ya wanachama wa upinzani kubambikiwa kesi.
Mbatia aliwataka wananchi wa Kata ya Nguruka kuachana na CCM kwa sababu imewatenga bila kuwaletea maendeleo kwa kipindi kirefu licha ya kukusanya kodi bila huruma kutoka mifukoni mwao.
Naye Mwenyekiti wa CHADEMA, alisema wakati wa kuungana na kuichukia CCM ili ing’oke madarakani umefika.
Aliwataka kukumbatia vyama vilivyo na nia ya kuwasaidia kuleta maendeleo, ambavyo sasa viko katika muungano.
Aliwatahadharisha kuwa iwapo wataendelea kuikumbatia CCM wataendelea kupigika miaka yote.
Ziara hiyo inafuatia ile iliyofanywa na Rais Kikwete na kudaiwa kupokea wenyeviti 73 wa Serikali za Mitaa kutoka CHADEMA.