ABIRIA 20 waliokuwa wakisafiri kutoka wilayani Monduli kuelekea mjini Arusha, wamefariki papo hapo baada ya gari walilokuwa wakisafiria kugongana uso kwa uso na lori.
Ajali hiyo ilitokea jana katika eneo la Meserani Dukabovu, Monduli, majira ya saa nane mchana baada ya gari hilo aina ya Hiace ‘Kipanya’, lenye namba za usajili T 776, ARH kugongana na lori lililokuwa limebeba mchanga.
Taarifa zilizopatikana kutoka kwa watu walioshuhudia tukio hilo na kuthibitishwa na Kamanda wa Polisi mkoani Arusha, Matei Basilio, zinasema kuwa, ajali hiyo ilitokea mara baada ya lori la mchanga lililokuwa likielekea Monduli, kutaka kulipita gari lililokuwa mbele yake na kusababisha ajali hiyo.
Ajali hiyo ilisababisha vifo vya abiria wote 20 waliokuwa kwenye Hiace, akiwemo dereva na kondakta wa gari hilo linalomilikiwa na Muhadi Yusuph, mkazi wa Sakina, Arusha.
Aidha, dereva wa lori lililosababisha ajali, lenye namba za usajili T 377 AGM mali ya Kampuni ya Pilazo Enterprise ya mjini Moshi, mkoani Kilimanjaro ambaye mpaka sasa jina lake halijafahamika, alikimbia.
Kwa mujibu wa kamanda wa polisi mkoani hapa, kazi ya kutambua marehemu waliokuwemo katika Hiace hiyo imekuwa ngumu kutokana na baadhi yao kukatika vibaya sehemu mbalimbali za viungo vya mwili.
Miili ya mabaki na mabaki ya viungo vya marehemu hao hadi jana jioni ilikuwa ikipelekwa katika Hospitali ya Mkoa ya Mount Meru kuhifadhiwa na kwa ajili ya utambuzi zaidi kutoka kwa ndugu na jamaa zao.
Kamanda Matei ametoa wito kwa wakazi wote wa mkoani Arusha na maeneo ya jirani, kwenda kutambua miili hiyo na kutaka ushirikiano kuwezesha kumkamata dereva wa lori lililosababisha ajali hiyo.
Wakati tunakwenda mitamboni, baadhi ya waliokufa walikuwa wameshatambuliwa. Hao ni Jimila Juma aliyekuwa dereva na Asifiwe Mohammed, kondakta wa gari hilo.
Abiria waliokufa ni Msee Kimarare, Tumai Deringo, Shazida Juma, Sebastian Sekaja, Stambuli Myovela na Msele Kimario ambao ni askari wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) kutoka Chuo cha Uongozi wa Kijeshi, TMA cha Monduli.
Wengine ni Amina Bitres, Omnyaki Lengoniki, Hamisi Mkumbo na mkewe aliyetajwa kuwa ni Mrs Mkumbo, Nakwetu Mengoriki, George Mashauri na Elibariki Mnzava. Mkumbo alikuwa amechaguliwa kuunda timu ya taifa ya mchezo wa Taekwondo.
Ajali hiyo imetokea ikiwa ni wiki moja na nusu tangu kutokea kwa ajali mbaya mkoani Singida iliyohusisha basi la Mohammed Trans, ambako abiria zaidi ya 25 walifariki katika ajali hiyo, na nyingine iliyotokea hivi karibuni na kuua abiria watatu mkoani Mbeya ikihusisha basi la Kampuni ya SABCO.