Na Mwandishi Wetu
MWANA Sanaa maarufu duniani wa Kimarekani, Franklin Gaskin, anayejulikana kwa jina la Franco the Great, anaingia Jijini Dar es Salaam kesho kwa ziara ya wiki moja kwa nia ya kutafuta njia ya kukuza utalii wa Tanzania nchi za nje kwa njia ya sanaa.
Ziara yake inatokana na mpango uliobuniwa na kampuni moja ya kitalii ya New York nchini Marekani iitwayo Time Warner Safaris ikishirikiiana na kampuni tatu za nchini Tanzania zinayojishughulisha na masuala ya utalii.
Habari zilizopatikana Jijini Dar es Salaam zinasema kampuni hizo ni Discover Tanzania Heritage inayosafirisha watalii, Stan Ad & Consultancy Ltd, ambayo inatoa chapisho maalum la Kili Album, kwa ridhaa ya Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) na Ujumbe Ink Ltd inayotangaza utalii kwa njia ya mtandao wa Internet.
Mtendaji Mkuu wa Time Warner Safaris, Bill Mushi, alisema Tanzania mpaka sasa ilikuwa haijachukua fursa mbadala ya kutangaza vivutio vyake vya utalii kwa njia ya sanaa. Utalii wa aina hii, alisema, umetokea kupendwa na umechangia sana mapato ya nchi mbalimbali.
Franco the Great, ambaye amewavutia watalii wengi kutembelea sehemu anayoishi Jijini New York, Harlem, amekubali kutengeneza michoro ya vivutio mbalimbali vya utalii vya Tanzania ambavyo vitaonyeshwa nchi za nje.
Mushi alisema ujio wa msanii huyo maarufu utasaidia kukuza utalii wa Tanzania kwa sababu umaarufu wa Franco umeenea katika nchi nyingi na ana uvuto wa kipekee.
Mkurugenzi Mtendaji wa Discover Tanzania Heritage, Saleh Dola, alisema kuwa akiwa nchini, Franco atatembelea mji mkongwe wa Bagamoyo, hifadhi ya Ngorongoro na hifadhi maarufu ya Serengeti ambayo hivi karibuni ilitangazwa kuwa mojawapo ya maajabu mapya duniani. Dola pia ni kiongozi wa asasi ya Bagamoyo Cultrural Heritage Tourism Cluster.
Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa na waandalizi, Franco pia anategemewa kukutana na Waziri wa Masliasili na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe, na viongozi wa Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) na hifadhi ya Ngorongoro na Bodi ya Utalii Tanzania.