WABUNGE wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), wameonywa kuwa makini wakati wakichangia hoja bungeni kwa kutoishambulia serikali.
Uamuzi huo ulifikiwa juzi usiku wakati wabunge hao walipokutana kama Kamati ya Chama kufanya tathmini ya namna walivyoshiriki katika kuchangia mjadala wa Hotuba za Bajeti na ile ya Mwelekeo wa Uchumi.
Moja ya michango iliyojadiliwa katika kikao hicho cha wabunge wa CCM ni ya Mbunge wa Nzega, Lucas Selelii, aliyetishia kukwamisha bajeti za wizara tatu ikiwamo ya Ofisi ya Waziri Mkuu akiishutumu serikali kwa kushindwa kutekeleza ahadi zake kwa muda mrefu.Wizara nyingine ambazo mbunge huyo katika mchango wake ametishia kuondoa shilingi ni pamoja na Wizara ya Miundombinu, akisema imeshindwa kutimiza ahadi ya ujenzi wa barabara katika maeneo mengi jimboni kwake.
Pia aliitaja Wizara ya Nishati na Madini ambayo imeahidi kwa muda mrefu kupeleka umeme katika vijiji kadhaa jimboni mwake, lakini hadi sasa hakuna kilichofanyika.
Vyanzo vyetu vya habari vya kuaminika ndani ya kikao hicho cha CCM, kilisema kikao hicho kilichoonekana kuwa ni cha kuwasuta baadhi ya wabunge wenye mdomo mkali dhidi ya serikali kiliongozwa na Waziri Mkuu, Edward Lowassa na Katibu Mkuu wa CCM, Yusuph Makamba.
“Jana tulikuwa na kikao cha wabunge wa CCM, Waziri Mkuu na Makamba walitumia muda mwingi kutusema, kwamba wabunge wa CCM tusiichambue serikali, tusiwe wasemaji sana. Sasa kwa hali hiyo sisi tumeamua kukaa kimya, tunawaachia wapinzani waseme,” kilisema chanzo chetu cha habari.
Baadhi ya wabunge wa CCM waliozungumza na Tanzania Daima walisema viongozi hao waliwaonya kuwa, michango yao inamchefua Rais Jakaya Kikwete.
Mmoja wa wabunge alisema endapo wabunge hao wataacha kuuhoji utekelezaji wa baadhi ya ahadi za serikali, hawataeleweka kwa wananchi na kwamba hali hiyo inaweza kuwaimarisha zaidi wapinzani.
“Sisi tuna miradi mingi ya maendeleo tuliyoahidi kutekeleza kwa wananchi wetu majimboni, ahadi hizo hadi sasa hatujatekeleza na mahala pakuuliza ni katika Bunge, sasa tufanye nini?” alihoji mmoja wa wabunge aliyehudhuria kikao hicho.
Vyanzo vyetu vya habari vilisema mara baada ya kikao hicho cha wabunge wa CCM, waliweka msimamo wa kutojadili bajeti za wizara mbalimbali.
Mbali ya Selelii, wabunge wengine waliotajwa kwenye kikao hicho kuwa michango yao ilikuwa mibaya kwa serikali ni Mbunge wa Bukoba Mjini, Balozi Khamis Kagasheki, ambaye katika mchango wake alidai kuwa Waziri Juma Ngasongwa wa Mipango na Uchumi na Uwezeshaji, alilidanganya Bunge kuhusu kujengwa kwa uzio katika Uwanja wa Ndege wa Bukoba.
Wabunge hao walisema, walijiandaa vya kutosha kujadili hotuba ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa madai kuwa ina mambo mengi ambayo wananchi wanapaswa kujua kupitia wabunge wao.