WAKIMBIZI zaidi ya 500 kutoka Somalia wamepewa uraia wa Tanzania baada ya kuishi nchini kwa miaka mingi.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani, Solomon Odunga, alibainisha hayo jana wakati wa maadhimisho ya Siku ya Wakimbizi Duniani yaliyofanyika katika viwanja vya Karimjee jijini Dar es Salaam.
Odunga alisema wakimbizi hao ambao wanaishi katika Kijiji cha Chogo, mkoani Tanga, walikimbia nchi yao kutokana na vita iliyokuwa ikiendelea na kujikuta wakiishi nchini miaka mingi kinyume cha sheria.
Alisema kutokana na taabu na mateso wanayoyapata wakimbizi kutoka nchi za Afrika ambazo zinaendelea na vita, ni dhahiri kuwa wanapaswa kusaidiwa ili waweze kuendesha maisha yao kama awali na kuwasaidia wengine kurudi makwao.
“Tatizo la wakimbizi si kuwasaidia kwa kuwapa nguo, chakula au kuwahifadhi sehemu, bali ni kuwasaidia ili waweze kurudi katika nchi zao... na ikibidi ni kuwapa uraia wale ambao wanaonekana wana sifa za kupewa,” alisema Odunga.
Alisema ili kulifanikisha jambo hilo, katika nchi nyingine jamii husika inapaswa kulaani vikali vitendo vyovyote vya kulazimisha kwa nguvu wakimbizi kwenda ugenini na badala yake kutoa mwito kukomesha vitendo kama hivyo.
Naye mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa Mtandao wa Mashirika ya Haki za Binadamu Kusini mwa Afrika, Israel Ilunde, akizungumza katika maadhimisho hayo alisema siku ya wakimbizi ni ishara ya kuheshimu taabu na mateso waliyopata wakimbizi.
Pia alisema siku hiyo inawapa moyo na kuunga mkono maombi na matumaini waliyonayo ya kuweza kurejea nchini kwao siku moja.
Siku ya wakimbizi duniani huadhimishwa kila Juni 20 ya kila mwaka na kaulimbiu ya mwaka huu ilikuwa: ‘Ninatamani kurudi nyumbani siku moja - hivi karibuni.’