WANAMUZIKI wakongwe katika medani ya muziki wa dansi nchini, Hassan Rehani Bitchuka na Zahir Ally Zorro, wanatarajiwa kufanya shoo ya pamoja katika Ukumbi wa Savoy mjini Morogoro, Juni 22.
Akizungumza jijini Dar es Salaam juzi, Mratibu wa onyesho hilo, Haruna Magea, ‘Dk. Kifimbo’ alisema shoo hiyo itakuwa ni maalumu kwa ajili ya kuutambulisha wimbo wao wa pamoja uitwao ‘Sheri Aisha’.
Dk. Kifimbo alisema wimbo huo ni ule waliouingiza katika shindano la muziki wa Kiafrika la Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC), mwaka jana.
Alisema sababu kubwa ya kuwaandalia onyesho maalumu wakongwe hao, ni kwa ajili ya kuwapa wakazi wa Morogoro burudani ambayo hawajaipata kwa muda mrefu.
“Unajua Zorro na Bitchuka ni watu muhimu katika medani ya muziki wa dansi Tanzania, na tuna kila sababu ya kuuenzi mchango wao, hivyo kwa sasa tunaandaa mpango wa kuwawezesha kutoa albamu yao, ndiyo maana unaona sasa tunawaandalia maonyesho sehemu mbalimbali,” alisema.
Mratibu huyo aliongeza kuwa, katika onyesho hilo, wanamuziki hao nyota, watapiga nyimbo walizotamba nazo enzi zao wakiwa na bendi mbalimbali.
Alisema Zorro atapiga nyimbo alizotamba nazo akiwa na bendi za JKT Kimulimuli ya Mafinga Iringa na Mass Media huku Bitchuka akiwakumbushia zile za enzi za NUTA, JUWATA hadi OTTU, Orchestra Safari Sound (OSS), DDC Mlimani Park ‘Sikinde’ zote za Dar es Salaam.
Dk. Kifimbo alisema onyesho hilo litasindikizwa na bendi ya muziki wa dansi ya Regent ya Morogoro.
Mratibu huyo alitoa wito kwa wakazi wa Morogoro, kujitokeza kwa wingi kuhudhuria onyesho hilo ambalo litakuwa ni la aina yake na la pekee kufanyika.