KAMBI ya vyama vya upinzani bungeni, imeitaka serikali kurudisha mara moja Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) kwa waagizaji wa mafuta nchini, kama ilivyokuwa awali.
Hatua ya kurudisha kodi hiyo, itasaidia kupunguza mzigo mzito kwa wananchi, ambao sasa wanaelekea kubaya zaidi kutokana na mwelekeo mpya wa serikali uliotangwaza kupitia bajeti yake, juzi.
Akizungumza na Tanzania Daima ofisini kwake mjini hapa jana, Kiongozi wa kambi ya upinzani bungeni, Hamad Rashid Mohammed, alisema hatua ya kurudisha VAT kwenye mafuta, itasaidia kuwapunguzia wananchi mzigo wa kupata mahitaji muhimu ya maisha.
“Sisi wapinzani tunasema, bajeti hii ni mbaya, na kwamba ili kuokoa hali za Watanzania wenzetu wenye kipato cha chini, ni kurudisha VAT kwenye mafuta iwe kama zamani,” alisema.
Alisema tangu serikali ilipoondoa VAT, matajiri wakubwa na waagizaji wa mafuta ndiyo wamekuwa wakineemeka zaidi kuliko wananchi kama ilivyokusudiwa.
“Tangu serikali ilipoondoa VAT na ushuru kwenye mafuta, matajiri wakubwa ndiyo wamekuwa wakinufaika zaidi kuliko walengwa, ambao ni wananchi wa kawaida... sisi tunasema hili lifanyiwe kazi mapema,” alisisitiza Rashid.
Alisema kambi ya upinzani inajiandaa kuwasilisha bajeti mbadala Jumatatu, ambayo itazingatia maslahi ya wananchi wa kawaida.
Alisema bajeti ya mwaka huu imeonekana kuongeza fedha nyingi katika utawala kuliko maeneo muhimu kama vile afya na kilimo.
“Hakuna ajira kubwa kwa Watanzania kama kilimo, lakini ukiangalia kwa makini utaona fedha zinazotengwa hazitoshi na nyingi zinapelekwa kwenye utawala,” alisema.
Kuhusu kupandishwa kwa gharama ya mafuta, Rashid alisema hiyo itawafanya wananchi wazidi kuwa ombaomba kutokana na kukosa fedha za kukidhi mahitaji.
Rashid alisema kama serikali ingekuwa makini katika sekta ya madini, ingeweza kuingiza fedha nyingi za kigeni, hali ambayo ingewapunguzia mzigo wananchi.
“Serikali imeshindwa kuwa makini katika sekta hii, kwani tumekuwa tukishuhudia mchanga unasafirishwa nje ya nchi kinyemela, huku makontena mengi yakikamatwa,” alisema.
Rashid, ambaye pia ni Mbunge wa Wawi (CUF), alisema mpaka sasa kuna kampuni nyingi zinazojishughulisha na uchimbaji wa madini zimemaliza mkataba wao, lakini serikali imekaa kimya bila kutoa taarifa yoyote juu ya kampuni hizo.
Alisema bajeti haikugusa maeneo muhimu kama vile utalii, uvuvi, uvunaji wa mazao ya misitu na magogo, sehemu ambazo zimekuwa zikiingiza fedha nyingi kwa taifa.
Naye Mbunge wa Buchosa, Samwel Chitalilo (CCM), alisema bajeti ya mwaka huu ni nzuri, lakini itasababisha maisha ya mwananchi wa kawaida kuwa magumu.
Alisema kitendo cha serikali kupandisha bei ya mafuta kitaendelea kuwaathiri wananchi wa vijijini, ambao wataendelea kuumia na kuharibu zaidi mazingira kwa kukata miti ovyo ili kujipatia kipato.
Baadhi ya wakazi wa mjini hapa waliozungumza na Tanzania Daima, walionekana kuwa na maoni tofauti kwa kusema kuwa sasa ugumu wa maisha umewadia.
Mmoja wa wakazi hao, Julius John, alisema kitendo cha serikali kuacha kupunguza bei za bidhaa kitasababisha kauli ya Rais Jakaya Kikwete ya maisha bora kwa kila Mtanzania kuwa kitendawili.
Naye Anna Mtimbuke, alisema serikali imeshindwa kuonyesha huruma yake kwa Watanzania.
Naye dereva teksi, Omar Shitwa, alisema kitendo cha serikali kuongeza gharama katika uingizaji wa magari nchini na kuongeza fedha katika leseni, kutasababisha tatizo la usafiri katika maeneo mbalimbali.