WATU wanaokadiriwa kufikia 20 wamepoteza maisha kwa kuteketea kwa moto baada ya basi la Kampuni ya Mohammed Trans kuanguka na baadaye kulipuka na kuteketea kwa moto.
Habari kutoka eneo la tukio zinaeleza kuwa, ajali hiyo ya aina yake ilitokea katika eneo la Kisaki lililo takriban kilometa 10 kutoka Singida Mjini.
Chanzo cha habari kutoka eneo la ajali kiliieleza Tanzania Daima kwamba, basi hilo lililokuwa na abiria wanaokadiriwa kufikia 60, lilikuwa likitokea Dar es Salaam kuelekea Mwanza.
Kwa mujibu wa chanzo hicho cha habari, ajali hiyo ilitokea baada ya magurudumu ya mbele ya basi hilo kupasuka kabla ya kupinduka na muda mfupi baadaye likalipuka.
Baadhi ya watu waliokuwa ndani ya basi hilo walifanikiwa kutoka wakijisaidia wenyewe na wengine wakipata msaada wa dharura kutoka kwa watu waliokuwa jirani.
Hata hivyo kazi hiyo ya uokoaji ilikwama baada ya basi hilo kulipuka hali ambayo ilisababisha waokoaji washindwe kuwanasua baadhi ya abiria.
Jitihada za waokoaji hao kuwanusuru abiria wengine waliokuwa wamenasa ndani ya basi hilo kwa kujaribu kuzima moto huo kwa kumwaga mchanga zilikwama.
Kukwama kwa juhudi hizo kulisababisha waokoaji hao wakate tamaa na hivyo kubaki wakiangalia basi hilo likiteketea kwa moto.
Habari zaidi kutoka eneo hilo zinaeleza kuwa, abiria wengine wanaokadiriwa kufikia 42 walionusurika katika tukio hilo walikimbizwa katika Hospitali ya Mkoa wa Singida kwa matibabu.
Watu waliozungumza na gazeti hili kutoka eneo la tukio, wanasema kuwa maiti wote waliobaki walikuwa wameteketea kwa moto na hivyo kusababisha upatikanaji wa miili kushindikana.
Habari zaidi zinasema kwamba, kutokana na tukio hilo, polisi wa mkoani hapa jana jioni walianza kuhakiki abiria wote waliokuwa wamepanda basi hilo ili kuweza kupata uhakika wa idadi kamili ya watu waliopoteza maisha yao.