BAADHI ya watu wmeonyesha wasiwasi wao iwapo ahadi zilizotolewa na serikali za kuwapunguzia ukali wa maisha zitatekelezeka ipasavyo, kutokana na ongezeko la kodi mbalimbali kupitia bajeti ya mwaka 2007/08.
Walionyesha wasiwasi huo jana mara baada ya Waziri wa Fedha, Zakia Meghji, kumaliza kuwasilisha bajeti hiyo bungeni.
Richard Mgaya, aliyejitambulisha kuwa ni mfanyabishara aliyeko Arusha, aliliambia gazeti hili kuwa, bajeti hiyo ina kasoro kubwa ya kushindwa kuelezea matumizi yatakavyokuwa.
Akizungumza na gazeti hili kwa simu, Mgaya alisema inafurahisha kuona kuwa serikali imeongeza bajeti yake hadi kufikia zaidi ya sh trilioni 6.
Lakini, alisema tatizo si kupata fedha, bali ni udhibiti wa matumizi.
“Nashangaa sana, katika hotuba yake waziri ameongelea kuhusu mapato tu. Vipi mbona hakugusia matumizi ya fedha tutakazokusanya?” alihoji.
Mgaya alisema kuwa, wasiwasi wake mkubwa ni jinsi fedha zitakazokusanywa kutokana na ongezeko la kodi zitakavypotumika.
“Tunaweza kujikuta tunakusanya fedha nyingi, lakini tunaweka katika mfuko ambao umetoboka kwa chini, hakitaeleweka kitu,” alisema.
Mfanyabishara mwingine, aliyejitambulisha kama mmiliki wa kituo cha kuuza mafuta, aliliambia gazeti hili kupitia ujumbe mfupi wa simu ya mkononi kuwa, ameshitushwa na ongezeko la ushuru wa mafuta.
Alikuwa akizungumzia ongezeko la ushuru wa mafuta lililotangazwa na Meghji jana la kutoka sh 100 kwa kila lita moja hadi sh 200, ambalo ni ongezeko la asilimia 100.
Katika bajeti hiyo, Meghji aliliambia Bunge kuwa, ili kuongeza uwezo wa Mfuko wa Barabara kumudu ongezeko la gharama za matengenezo ya barabara, serikali inapendekeza kuongeza ushuru wa mafuta ya petroli kutoka sh 100 za sasa kwa lita hadi sh 200 kwa lita.
“Tangia lini ukasikia kodi ya mafuta ya road toll (ushuru wa barabara) ikapanda kwa asilimia 100?” alihoji mfanyabishara huyo ambaye pia ni msafirishaji.