MRATIBU wa Kampuni ya Ukraine Education Fund, Dk. Noordian Jella, ameishangaa serikali kwa kuwakana wanafunzi wa Kitanzania wanaosota nchini Ukraine kutokana na kushindwa kulipia gharama za masomo yao.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Dk. Jella alisema kuwa wanafunzi hao waliondoka nchini wakiwa na baraka zote za serikali.
Alisema wanafunzi waliokwama Ukraine waliondoka kwa baraka zote za serikali na Bodi ya Mikopo.
Aidha, alisema kuwa waliondoka baada ya kuhakikishiwa na Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu nchini kuwa watapatiwa mikopo wanayoihitaji kwa ajili ya masomo yao ughaibuni.
Dk. Jella aliyasema hayo jana katika Ukumbi wa Idara ya Habari (MAELEZO) alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari.
“Mimi ndiye mratibu wa mpango mzima wa vijana hawa kusoma huko na nilikuwa kiunganishi kati ya vyuo wanavyosoma na Bodi ya Mikopo,” alisema.
Aidha, alisema kuwa anasikitika kuona Bodi ya Mikopo na Wizara ya Elimu ya Juu, Sayansi na Teknolojia wakiwa na msimamo tofauti wa kutowatambua vijana hao na kutokuwa tayari kuwasikiliza na kuwapa kile ambacho ni haki yao.
“Mimi binafsi na wanafunzi hawa 29 na wengine 84 ambao walitangulia hatuoni ajabu kwa msimamo huu wa serikali, kwani tangu zoezi la wanafunzi kwenda kusoma Ukraine lianze 2005, kumekuwa na pingamizi za aina mbalimbali kutoka Wizara ya Elimu ya Juu na Bodi ya Mikopo, kwani wamekuwa wakibaguliwa kana kwamba Watanzania hawatakiwi kusoma Ukraine,” alisema.
Aidha, alidai kuwa wapo baadhi ya wanafunzi waliochaguliwa kwenye vyuo vingine vya nje na kupewa mikopo wakati vyuo hivyo havina hata usajili, walimu na madarasa ya kutosha.
“Inashangaza kuwa wanaosoma katika vyuo kama hivyo visivyotambulika rasmi, wamepewa mikopo, tena wengine mara tano ya wale wa Ukraine,” alisema Dk. Jella.
Alisema wanafunzi hao wanapatwa na matatizo hayo kutokana na vita anayopigwa yeye na baadhi ya maofisa wa wizara na bodi, ambao walishawahi kupelekeana ujumbe kupitia simu kuwa wahakikishe hapeleki wanafunzi Ukraine hadi akubaliane na masharti yao.
“Mwaka jana Wizara ya Elimu ya Juu ilibadilisha utaratibu wa kutoa mikopo na walitoa masharti magumu ya kutotoa mikopo kwa wanafunzi wa nje ya nchi isipokuwa tu kwa nchi zilizo na gharama nafuu, kwa kisingizio kwamba hawana pesa, lakini cha kushangaza wizara imepeleka wanafunzi 93 katika nchi tatu, China, India na Algeria, na wanafunzi hao wamepewa kila mmoja sh milioni 10,” alidai.
Alisema tofauti na gharama hizo kubwa, kila mmoja kati ya wanafunzi waliopo Ukraine, anahitaji wastani wa sh milioni tatu tu.
“Pamoja na kubadilika kwa utoaji wa mikopo, hakuna hata kipengele kimoja kilichowataja wanafunzi 29 ambao walikubaliwa kupewa mikopo kabla ya kuahirisha masomo,” alisema.
Alisema baada ya kufika mwaka mwingine wa masomo, alikwenda wizarani kuthibitisha iwapo wanatakiwa kujaza tena fomu za kuomba mikopo lakini mkurugenzi mtendaji wa Bodi ya Mikopo, akasema kuwa hawana haja ya kujaza tena fomu hizo kwa kuwa walishakubaliwa kupata mikopo tangu mwaka uliotangulia.