Na Ramadhan Semtawa
WAKATI Bunge la bajeti likianza kesho mjini Dodoma, hatima ya Shirika la Posta Tanzania (TPC) na Shirika la Ndege Tanzania (ATCL), bado haijafahamika kutokana na bajeti ya Wizara ya Miundombinu, kushindwa kuonyesha kiasi cha fedha kilichotengwa kwa ajili ya kunusuru mashirika hayo.
ATCL hadi sasa ina ndege tatu, mbili zikiwa za kukodi huku TPC ikihitaji kufutiwa deni la mamilioni ya fedha ambalo linahakikiwa huku ikihitaji kupatiwa mtaji.
Mkazo wa sehemu kubwa ya bajeti ya Wizara ya Miundombinu ya mwaka huu, unaelekezwa katika miradi ya barabara ikiwa ni pamoja na kulipa deni la sasa la Sh93 bilioni.
Kwa mantiki hiyo, kama bajeti ya wizara hiyo itakwenda kama ilivyodokezwa na Waziri wake, Andrew Chenge, wiki iliyopita, basi mashirika hayo yataendelea kuwa katika hali ngumu na kutishia ustawi wao.
Hata hivyo, mwishoni mwa wiki baada ya kuelezwa wizara hiyo imeongezewa asilimia 15 katika bajeti yake kutoka katika fedha za matumizi ya kawaida ya kila wizara, mmoja wa wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Miundombinu, aliliambia gazeti hili kwamba, ATCL ilikuwa imetengewa Sh20 bilioni kama sehemu ya kuanza kununua ndege mpya, lakini ikiwa haijafahamika ni ya aina gani na ukubwa kiasi gani.
Alipoulizwa Chenge, kuhusu hilo, alisema " Hadi sasa haijafahamika, mtazamo ni kwamba ATCL huenda itaendelea kukodisha ndege, kununua ndege mpya si kitu kidogo kama unavyokwenda dukani kununua shati."
Kwa upande wa TPC, wafanyakazi wa shirika hilo kwa ushirikiano na Chama cha Wafanyakazi wa Sekta ya Mawasiliano na Uchukuzi (Cotwu), katika taarifa yao kwa kamati ya miundombinu, walisema hakuna juhudi za dhati za kulinusuru shirika.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka kwa mmoja wa wajumbe wa Cotwu, hadi sasa kamati ya miundombinu na serikali hazijaonyesha nia ya dhati ya kulinusuru shirika.
"Makubaliano ya kikao cha baraza la wafanyakazi na chama, hadi sasa inaonekana hakuna juhudi za dhati za kulifanyia marekebisho shirika," ilisema sehemu ya taarifa hiyo.
Hata hivyo, majadiliano ya baadaye kati ya kamati na wawakilishi hao, yalitoa majibu ya kutaka marekebisho ya shirika yatekelezwe kwa kasi.
Hata hivyo, hadi sasa suala la shirika kufutiwa madeni yake na kupewa mtaji ili lijiendeshe upya limebaki kuwa chini ya kamati maalum ya makatibu wakuu watatu wa wizara.
Juhudi za kunusuru TPC, zinafanywa na kamati maalum inayoundwa na makatibu wakuu kutoka miundombinu, mipango uchumi na uwezeshaji, fedha na Mwenyekiti wa Tume ya Rais ya Kurekebisha Mashirika ya Umma (PSRC).
Chenge akizungumzia zaidi, alisema kwa upande wa ATC, inaweza kutumia ndege hizo za kukodi huku kukiwa na mipango ya kupata ndege mpya.
Chenge alisema taratibu za kununua ndege zinaruhusu kuweka kiasi fulani cha fedha kabla ya kununua ndege mpya.
"Kama ndege zingekuwa zinanunuliwa kwa urahisi tu kama shati sawa, ndege ni gharama, lakini kuna taratibu hata kama huna fedha taslimu unaweza kuwekeza kiasi fulani, ndiyo maana hadi sasa tunachotafuta ni fedha," alisema.
Alisema azma ya serikali ni kuona ATCL inajiendesha kwa ufanisi mkubwa ili imudu ushindani.
Kuhusu TPC, wiki iliyopita Naibu Waziri wa Miundombinu, Dk Maua Daftari, aliliambia gazeti hili ofisini kwake kwamba, alikuwa akisubiri kamati ipeleke hatua ya mchakato ulipofikia.
"Juhudi zinafanyika, ila sisi hadi kamati ituletee maelezo, lakini hatua zinafayika kweli," alisisitiza Dk Maua.