VIONGOZI wa vyama vya upinzani wamedai kuwa, kauli za Rais Jakaya Kikwete kutochunguza tuhuma zinazomkabili mtangulizi wake, Rais mstaafu Benjamin Mkapa, anayedaiwa kufanya biashara wakati akiwa Ikulu, ni dalili kuwa hata naye si msafi.
Wapinzani waliyasema hayo jana, katika mkutano wao wa pamoja, kupitia tamko ambalo kwa kiasi kikubwa lilisomwa na Mwenyekiti wa Tanzania Labour Party (TLP), Augustine Mrema.
Katika tamko hilo, Mrema alidai kuwa, kitendo cha Rais Kikwete kuwataka waandishi wa habari kuachana na tabia ya kuwachunguza viongozi wastaafu, hususani katika masuala madogo, ni tuhuma kwake na anakiri kwamba wanaoingia Ikulu wote si wasafi, isipokuwa baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere.
Alisema kitendo cha Mkapa kuchukua mkopo, kinaonyesha wazi kuwa alitumia dhamana ya urais na hiyo ni sawa na kuwaweka rehani Watanzania.
Aidha, Mrema alisema kitendo hicho si cha kunyamaziwa, hasa ukizingatia kuwa Mwalimu Nyerere alishawahi kusema kuwa Ikulu si mahali pa kufanyia biashara.
Mrema alidai kuwa, kilichofanywa na Mkapa ni dhambi kwa Watanzania na madhara ya kumtetea sasa, yataonekana baadaye.
Alisema ikiwa wakati anaingia madarakani, Mkapa alitangaza mali alizonazo, pamoja na kiasi cha fedha ambazo alikuwa ameziweka katika akaunti yake, ili kuweka imani kwa wananchi, alipaswa kufanya hivyo wakati alipokuwa akiwa amestaafu.
“Kwa kuwa sera yake ni ya uwazi na ukweli, atangaze hivi sasa alivyoondoka navyo, ili Watanzania tujue na tuache kumzungumzia kwa kumuonea,” alisema Mrema.
Aidha, walizungumzia pia wimbi la viongozi wa upinzani kuhamia Chama Cha Mapinduzi (CCM) na kudai kuwa hizo ni mbinu za kuua upinzani nchini.
Akitoa mifano, alisema kuwa alipokuwa ziarani Kigoma hivi karibuni, Rais Kikwete aliitumia mikutano yake kukipigia debe chama anachokiongoza wakati ziara hiyo ilikuwa ni ya kiserikali.
Akisoma tamko hilo la wapinzani, Mrema alisema Rais Kikwete alikwenda katika mikoa ya Kigoma na Rukwa na kutumia mikutano ya kiserikali kuvibomoa vyama vya upinzani na kwamba hawatakivumilia kitendo hicho.
“Kitendo alichokifanya ni kutubomoa, hivyo sisi kama viongozi wa upinzani hatukikubali, hatukivumilii kwa kuwa si cha kistaarabu kwa mpenda demokrasia yeyote yule,” alisisitiza.
Mrema alisema rais, mbunge, diwani au mwenyekiti anapoitisha mkutano wa hadhara kikazi, ni wa watu wote na si wa chama chake cha siasa na ni kwa ajili ya kueleza wananchi shughuli za maendeleo.
Alisema jumla ya wanachama 669 walijiunga na CCM wakati wa ziara ya Rais Kikwete mkoani Kigoma na wengi wao walikuwa ni viongozi wa CHADEMA.
“Habari hii si njema kwa taifa letu na kwa ustawi wa demokrasia kwa ujumla. Hili linahatarisha ustawi wa vyama ambavyo vinajiendesha kwa mujibu wa sheria halali za nchi,” alisema.
Mrema alisema hilo linaonyesha tabia tatu za Rais Kikwete alizozitaja kuwa ni kutokuwa makini, ukosefu wa utawala bora na uvunjaji wa katiba.
Alisema Kikwete ameonyesha hayo kutokana na kauli aliyowahi kuitoa awali kuwa, hana nia wala sera za kuua upinzani.
“Lakini kwa kitendo cha kuwapokea wenyeviti 73 wa Serikali za Mitaa toka CHADEMA, huku akichekelea, hakiwezi kuitwa jina lingine, isipokuwa ugeukaji wa kauli zake,” alisema Mrema.
Akifafanua ukosefu wa utawala bora, alisema utawala wowote ule ili uweze kushinda vigezo vya utawala bora, ni lazima uheshimu mamlaka na ngazi za utawala na uongozi mwingine, hata kama utawala huo na uongozi huo hauko chini yake.
Aliongeza kuwa, rais amevunja katiba kwa kudai kuwa CHADEMA haina serikali, wakati Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa ni wa CHADEMA.
Wakati huo huo, viongozi hao wa upinzani walimpongeza Rais Kikwete kwa kampeni yake ya kuhamasisha kupima ukimwi kwa hiari, na kumuomba ifikapo tarehe 14 yeye awe wa kwanza katika kuongoza upimaji huo, nao watakuwepo kumuunga mkono.