KAMATI ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa, jana ilikataa kupokea ripoti za mwaka za Halmashauri tatu kutoka Mkoa wa Kigoma kwa madai ya kutokuwa na ufafanuzi wa kutosha.
Halmashauri ambazo taarifa zake zimekataliwa na kamati hiyo ni Kigoma Vijijini, Kibondo na Kigoma Ujiji.
Hoja za kukataa taarifa hizo zilimetokana na mkanganyiko wa vitabu vya mahesabu ya halmashauri hizo, ambavyo vimetofautiana na vilivyopelekwa kwa mkaguzi.
Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mgana Msindai (Iramba Mashariki-CCM), alisema sababu ya kukataa taarifa za halmashauri hizo ni ugeni wa wakurugenzi wa halmashauri hizo.
Alisema wakurugenzi waliohamishwa wana taarifa na maelezo mazuri zaidi kwa kuwa hao waliohamishwa ndio walioandaa taarifa hizo.
Aliongeza kuwa wajumbe wa kamati wanahitaji zaidi kufahamu hatua zinazochukuliwa na halmashauri hizo katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo.
Lakini wakurugenzi wapya hawana taarifa za kina kuhusiana na miradi hiyo kwa hiyo kuanza kuwahoji maswali kuhusiana nayo, ni sawa na kuwaonea.
Alisema: “Wakurugenzi karibu wote wa Kigoma ni wageni, ndiyo maana tumekataa taarifa zao ili kuwapa muda wa kujipanga na kutembelea miradi ya maendeleo ili watakapokuja wakiulizwa swali wasikose majibu.
“Kawaida huwezi kutoa maelezo ya kutosha kuhusu taarifa ambayo hujaiandaa wewe… mfano mzuri mmoja kati ya wakurugenzi tuliokataa taarifa zao alianza kazi Mei 29 mwaka huu, sasa huyu hana majibu ya kutosha kuhusu halmashauri yake,” alisema.
Alisema kamati imewapa muda wa kutosha kutembelea miradi mbalimbali inayotekelezwa na halmashauri zao na kueleza kuwa watakutana na wakurugenzi hao baada ya kikao kijacho cha Bunge na kuwataka wawe na majibu ya kutosha.
“Waheshimiwa wabunge walitembelea maeneo mbalimbali ya miradi ya maendeleo mkoani Kigoma hivyo wana maswali mengi ambayo wageni hao wasingeweza kujibu…huyo anayesema mengine shauri yake mimi ndiye mwenyekiti wa kamati na yaliyojiri ni hayo,” alisema Masindai.
Mkoa wa Kigoma una jumla ya halmashauri nne, ambazo ni Kigoma Ujiji, Kibondo, Kasulu na Kigoma Vijijini.