WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira), Profesa Mark Mwandosya, amesema yuko tayari kukabiliana na washindani wake kisiasa, katika uchaguzi wa viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Amesema, anaamini wananchi wa Mbeya hawamchukii na kujitokeza kwa wanachama wengi kuwania wadhifa anaoushikilia wa ujumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa mkoani hapa, ni msukumo walionao wa kutaka kukitumikia chama chao.
Akizungumza na Tanzania Daima hivi karibuni mkoani hapa, Profesa Mwandosya alisema, makundi yaliyoibuka sasa, ambayo kwa kiasi kikubwa yanasambaza fitina kwa baadhi ya wagombea, yanapaswa kupigwa vita kwa sababu yanahatarisha uhai wa chama mkoani hapa.
Alisema haamini kama kujitokeza kwa wanachama wengine kuwania nafasi hiyo anayoishikilia, kunatokana na chuki iliyojengeka kwa baadhi ya washindani wake wa kisiasa baada ya kutoa ushindani mkubwa katika kuwania kuteuliwa kuwa mgombea urais kupitia CCM dhidi ya wagombea wengine aliokuwa akichuana nao, kama inavyoenezwa na baadhi ya watu.
Alisema anaamini kuwa kujitokeza kwa wanaCCM wengi kuwania nafasi mbalimbali za uongozi katika chama hicho, ikiwemo ya ujumbe wa NEC, kunatokana na ari waliyonayo kukitumikia chama.
Alisema kwa maana hiyo, ni wanaCCM watakaoamua ni nani wanafaa kuwa viongozi katika kipindi hiki cha kukijenga upya chama.
“Hakuna sababu ya yote haya kutokea, vijimaneno na makundi makundi ni lazima sasa tuviepuke kama tunataka kujenga chama imara na kinachoheshimu kweli demokrasia.
“Jambo la msingi kwa sasa ni umoja na mshikamano ndani ya chama, kuanzia kwa wanachama hadi viongozi.
“Unajua, ukisema kuwa una viongozi wa kitaifa walio bora, maana yake ni kuwa ulisimamia vema uchaguzi kuanzia ngazi ya shina hadi ngazi hii, ambayo sisi wengine tumechukua, hivyo nafasi hii si ya kupotezwa na wanachama, ni muhimu wakachagua viongozi wenye uwezo kweli wa kuongoza.
“Uchaguzi wa sasa, ni tofauti na huo unaosemwa wa urais, mwaka juzi, uchaguzi huu ni wa kukijenga chama kwa kuchagua viongozi wanaofaa na si bora kiongozi, wanaCCM wanapaswa kufanya maamuzi yao ya kuchagua watu wanaowataka kukiongoza chama kwa kufuata kanuni na taratibu za chama, ambazo naamini ni bora kupita vyama vyote nchini,” alisema Profesa Mwandosya.
Alisema kitendo cha kujitokeza kwa wanaCCM wenzake kuwania wadhifa anaoushikilia, hakikumshtua kwa sababu ni jambo la kawaida katika uchaguzi wa aina yoyote kuwepo ushindani, na uchaguzi usiokuwa na ushindani hauna nafasi katika zama za sasa.
Hata hivyo, alionya kuwa, wanaCCM wanapaswa kuwa makini na watu wanaotaka kuutumia uchaguzi huo kuchochea mifarakano kwa kuhusisha mambo yasiyostahili kuwepo katika uchaguzi huo.
Alisisitiza kuwa, uchaguzi ndani ya chama ni changamoto muhimu za kuleta maendeleo, na haupaswi kutumiwa kupoteza mwelekeo mzima wa kuwapo kwa zoezi hilo.
Profesa Mwandosya alisema kuwa, ameamua kuwania tena nafasi hiyo kubwa katika chama, ili kusaidiana na wananchi mkoani Mbeya kutafuta maendeleo kwa njia shirikishi, ambapo kwa kufanya hivyo, uimara wa chama uonekana.