SERIKALI imeombwa kuongeza fedha za ruzuku kwenye shule za sekondari wilayani Kilombero.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti, walimu wakuu wa shule za sekondari za Kilombero, Kiyongwile na Ifakara, waliliambia gazeti hili kuwa, fedha zinazotolewa na serikali hazitoshelezi.
Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Kata ya Kiyongwile, Thomas Chihwalo, alisema fedha za fidia na ruzuku wanapata, lakini hazitoshelezi, na kwamba zimekuwa zikichelewa mara kwa mara hali inayosababisha uendeshaji kuwa mgumu.
Naye Mkuu wa Shule ya Sekondari Kilombero, Engelbert Matupa, alikiri kuwepo kwa tatizo hilo na kusema kuwa, kutokana na fedha hizo kutotosheleza, wakati mwingine wamekuwa wakiwaambia wazazi wa watoto wanaoanza kidato cha kwanza au kuhamia kuchangia sh 35,000 kwa ajili ya kununulia madawati.
“Fedha zinakuja, lakini hazitoshelezi na zimekuwa zikichelewa… unapokosa fedha uendeshaji unakuwa mgumu, kwani wakati mwingine wanafunzi wanapaswa kwenda kwenye safari za kitaaluma, lakini inashindikana,” alisema.
Wakati huohuo, baadhi ya walimu wilayani humo wamelalamikia ahadi walizoziita za uongo za serikali.
Akizungumza na gazeti hili, mmoja wa walimu hao, Zulfa Mtumwa, alisema serikali imekuwa ikiwaahidi walimu wanaokwenda kufundisha kuwa itawapatia fedha za kujikimu pamoja na mishahara ya miezi miwili, lakini badala yake wanapokuwa wamekwenda sehemu walizopangiwa, hawakuti fedha.
Kutokana na hali hiyo, alisema walimu wengi, hasa wale wageni na maeneo waliyopangiwa, wamejikuta wakiishi katika mazingira magumu, na wakati mwingine wanalazimika kuishi kwa kukopa.