Kitaifa
   Siasa
   Jamii
   Uchumi
   Makala

 

Search


Advanced Search

 »  Home  »  Habari za Kitaifa  »  Mkapa kavunja mwiko, Ikulu si patakatifu tena
Mkapa kavunja mwiko, Ikulu si patakatifu tena
By Habari Tanzania | Published  05/30/2007 | Habari za Kitaifa | Unrated

ILE kashfa ya ununuzi wa rada ilipokuwa imevuma wakati Rais Benjamin Mkapa akiwa madarakani, watu hawakuonekana kuhoji sana jinsi rais wao alivyokuwa akitumia muda wake wa kuwa ikulu.

Pengine hawakuwa na taarifa za kutosha au waliona kuwa ilikuwa mapema mno.

Tulimwona Waziri wa Mambo ya Nje wa Uingereza, Clare Short, akija Tanzania akiwa amenuna; baada ya kuwa amehoji sana ‘deal’ hiyo ya rada na kuipinga kwa nguvu zake zote.

Kutoka Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Dar es Salaam (sasa ‘wa Julius Nyerere’) alikwenda Ikulu.

Kina sisi tulibaki nje tukisubiri atakachosema atakapotoka huko kulikokuwa na kile kilichoitwa ‘mazungumzo ya faragha’ na viongozi wetu.

Kwa mshangao wetu, aliingia amenuna lakini akatoka anacheka. Alisema suala la rada wamelizungumza kwa kirefu na ‘ameelewa’. Akapanda ndege akaenda zake.

Huyu ni Waziri wa Uingereza aliyekuwa akipinga mpango wa Tanzania kununua rada kwa bei kubwa.

Binafsi niliwaza: “Viongozi wanazungumza lugha moja. Na kinachoweza kuzungumzwa kwenye magazeti si kile kinachoweza kuzungumzwa faraghani.

Kwa suala nyeti na la kiusalama kama la rada linaweza kuwa na maelezo ya kuridhisha zaidi faraghani, ndiyo maana wazee wameelewana. Sisi watu wa magazeti tusiwe na nongwa.”

Hata hivyo, majuzi tumepata habari za kushitusha: Kwamba ununuzi ule wa rada ulikuwa umegubikwa na lindi la rushwa. Uchunguzi umeonyesha kuwa wakubwa walikuwa wamechukua ‘cha juu’ kuuziwa rada kwa bei kubwa kupita kiasi.

Uingereza imefanya uchunguzi wake na kugundua ulaji wa kutisha. Nchi yetu imekuwa ikitafunwa na wenye meno.

Kutokana na hili, wapo waliomtaka aliyekuwa rais wakati huo ajibu maswali yetu kuhusu kashfa hii. Walikuwa na haki ya kufanya hivyo.

Mrithi wake, Rais Jakaya Kikwete akaja juu: “Hivi jamani kweli mnamtaka mzee Mkapa atoke huko aliko aje ajieleze? Ajieleze nini? Hebu mwacheni mzee wa watu apumzike!” aligomba Rais Kikwete.

Kwangu mimi sikuona mantiki yake. Na mtoa hoja hakuieleza. Alitumia zaidi hisia: Kwamba ‘mzee Mkapa aachwe apumzike’.

Nilitarajia Rais Kikwete aseme kwa nini Rais wa Awamu ya Tatu asijieleze kwetu jinsi alivyotumia dhamana tuliyompa? Alitakiwa aseme kwa nini Benjamin Mkapa asitoe maelezo juu ya watu walio chini yake kupokea hongo na kuhatarisha taifa?

Na alitakiwa aseme kwa nini mzee Mkapa asihusishwe na kashfa ya rada. Kama haya yangekuwa si lazima kutoka kwa Mkapa, angeyatoa yeye mrithi wake aliyemkingia kifua. Hakuna lililofanyika. Tukanyamaza.

Mengi yalitufanya tunyamaze. Mojawapo ni kuwa Rais Kikwete alisema Uingereza bado wanachunguza kwa kina suala hilo na kwamba tutadai ‘chenji’ yetu iliyozidi katika ununuzi ule ambao umedaiwa kuwa ulikuwa na bei kubwa kupita kiwango.

Lakini kwa hili la watumishi wetu serikalini kupokea hongo tumenyamaza kwa kuwa sisi ni Watanzania. Tunaodumisha ‘amani na utulivu’.

Ni lazima tunyamaze ili tuwe na amani. Amani kama ya makaburini ambako, tofauti na sokoni, kuna ukimya mkuu na utulivu. Nani apige kelele?

Leo kumezuka suala jingine zito sana. Kwamba akiwa Ikulu, Rais wa Tanzania alisajili kampuni ya biashara na kuendelea kufanya biashara huku akikopa katika benki kadhaa hapa nchini.

Tangu mwaka 1999, Benjamin Mkapa na mkewe Anna, walikuwa wakurugenzi wa ANBEM Limited. Lakini hawakuwahi kujitokeza hadharani kama wafanyabiashara, ila tulimjua mzee Mkapa kama rais na mkewe Anna kama mwanaharakati wa ukombozi wa wanawake akiongoza Taasisi ya Fursa Sawa kwa Wote (EOTF).

Tunataka maelezo kutoka kwa mzee Mkapa. Na katika hili, tunamuomba Rais Kikwete akae pembeni. Asimkingie kifua. Tunataka atueleze japo kwa kifupi sana kwa nini alitumia muda aliokuwa ikulu kufanya biashara?
Tunataka aseme kwa nini ANBEM Limited iliyoanzishwa ikulu na kuendeshwa na rais aliyeko madarakani huku ikiwa kampuni binafsi isifilisiwe na kurudishwa kwa wananchi.

Habari kwamba tangu mwaka 1999 watu wawili walikuwa wakiendesha kampuni binafsi ya biashara kutoka ikulu ya Tanzania si habari ndogo.

Pamoja na kuwa sisi tunaweza kuwa ‘wavivu wa kufikiri’, ‘malofa’ na ‘waandishi uchwara’, lakini tunahitaji majibu yenye hoja nzito kutoka kwa Benjamin Mkapa.

Habari zinasema Juni 21, 1999, mwaka aliofariki Mwalimu Julius Nyerere, Benjamin Mkapa na mkewe Anna walisajili kampuni binafsi iitwayo ANBEM Limited.

Kampuni hiyo ilipata hati ya usajili yenye namba 36547. Ilipofika mwaka 2005, wakati Mkapa alipokuwa anastaafu urais, kampuni yake ilikuwa na madeni yanayofikia kiasi cha shilingi milioni 750, zilizokopwa kutoka benki mbalimbali.

Swali ni kwamba, Rais wa Tanzania aliwezaje kuwa mfanyabiashara mkubwa kiasi hicho bila kuwapo kwa mgongano wa masilahi dhidi ya washindani wake kibiashara? Mikopo hii kutoka benki mbalimbali hapa nchini ilipatikana kati ya Julai na Desemba 2002 wakati Mkapa alipokuwa bado Rais wa Tanzania, je, iliwezekana kumtenganisha Benjamin Mkapa na madaraka ya urais walipokwenda kuomba mkopo?

Rais Mkapa alitangaza mali zake alipokuwa akiingia madarakani, lakini hakufanya hivyo alipokuwa akiondoka, licha ya watu wengi kumtaka atangaze ili tujue kama ametumia ikulu kujineemesha.

Anapokuwa madarakani, rais ni kiongozi wa wote na ndiyo maana anaangaliwa kwa kila kitu ili awe mtu huru asiyehangaika.

Anapaswa kuwa mwamuzi kati ya watu wanaogongana wakati wakitafuta riziki. Hapaswi kuwa naye mtafutaji anayegongana na watafutaji wenzake huko.

Ndiyo maana Mwalimu Julius Nyerere aliwahi kutuasa kuwa ikulu ni mahali patakatifu na si pa kufanya biashara.

Je, haitakuwa sahihi kutamka kwamba, Ben alivunja mwiko huo na kupafanya ikulu mahali pa kufanyia biashara?

Mwalimu alishangaa kwamba katika miaka yake 23 ya kukaa ikulu hakuona biashara yoyote lakini watu walionekana kuwa tayari kutumia fedha kuitafuta ikulu.

Hapa alimaanisha kuwa, ni dhambi kwa mtu tuliyemweka ikulu kufanya biashara kwa kuwa si mahali pake.

Nakumbuka wakati wa uongozi wake, Rais Mkapa alikwenda nchini Malawi alikokutana na kiongozi wa huko, Bakili Muluzi, kati ya mengi aliyoyasema pia alisema kuwa kuna dhana miongoni mwa Waafrika kuwa kiongozi bora anastaafu akiwa maskini.

Alipingana na dhana hii na kusema kuwa si dhana sahihi. Nami nilikubaliana naye wakati ule na ninakubaliana naye sasa, lakini sikubaliani na dhana ya kiongozi kutumia muda wake wa ikulu kufanya biashara binafsi. Pengine nina mning’inio wa Azimio la Arusha.

Ni vigumu kumtenganisha mtu na cheo chake, hivyo Mkurugenzi wa ANBEM Limited anapoomba mkopo papo hapo akiwa Rais wa Tanzania, anakuwa juu ya waombaji wengine, na kwamba ikiwa fursa ni chache, basi mkopo utatolewa kwa ANBEM na si kampuni nyingine. Hii ni kibinadamu.

Viongozi wetu wamevunja Azimio la Arusha lililokuwa limeweka misingi ya kiutu katika uhusiano wa kijamii na maadili ya uongozi. Hili tunalijua. Je, ina maana kuwa tumeua kabisa maadili ya uongozi katika nchi hii?
Lakini pamoja na kwamba Azimio la Arusha halipo tena, nadhani bado tunahitaji rais atakayekuwa hana upande wakati tunapogombania mkate wa kila siku na si mtu anayenyang’anyana nasi uwanjani.

Kwa rais kukaa ikulu kabla ya kwisha kipindi cha kwanza akasajili kampuni ya biashara, na pia akaingia tena katika kinyang’anyiro cha urais; akaomba mkopo benki na kuendesha biashara yake kutoka ikulu, tunahitaji maelezo.

kidanka@hotmail.com


How would you rate the quality of this article?
1 2 3 4 5
Poor Excellent
Add comment
Comments
  • Comment #1 (Posted by an unknown user)
    Rating
    very good news, this is what Tanzanian need to know THE TRUTH about people in Power.. most of our leaders think to be in power means people to work for them not they are suppose to work for the people..and all they think is they can do what they want and get away with it.
     
Submit Comment


Article Options
Your Favorite Articles
View All Favorites
Articles to Read
You Recently Viewed...
Popular Articles
  1. Unaifahamu Jambo Forums?
  2. Barua ya Wazi kwa Rais Jakaya Kikwete
  3. Ghorofa Jijini lanusurika kuungua moto
  4. Is Tanzania a safe place to invest?
  5. Britsh M.P. calls for the suspension of aid to Tanzania.
No popular articles found.
Popular Authors
  1. Habari Tanzania
  2. Mzee Mwanakijiji
  3. Marshy Abdu
  4. Linda Garner
  5. Nthelezi Nesaa
  6. Prosper Kwigize
  7. Ramadhan Semtawa
  8. Salehe Mmoro
  9. Manyerere Jackton
  10. Ndesanjo Macha
No popular authors found.