HOJA ya nani arithi mikoba ya aliyekuwa kocha mkuu wa timu ya Simba, Mbrazil, Nielsen Elias, kwa sasa inawaumiza vichwa viongozi wa klabu hiyo.
Habari kutoka ndani ya klabu hiyo, zinasema, katika kujadili nani wa kuvaa ‘viatu’ hivyo, juzi na jana viongozi wa klabu hiyo walikutana kujadili bila kupata jawabu.
Kitu kinachowaumiza kichwa, ni suala la gharama kubwa zinazohitajika kwa kocha wa kigeni, hivyo kama atapatikana, itachukua muda mrefu kiasi.
Wakati wakitafakari hilo, kabla ya kukamilika kwa mipango ya kocha wa kigeni, wanatafuta ni nani akamate kwa muda nafasi hiyo ya kocha mkuu.
Kwa mujibu wa habari kutoka ndani ya Simba, kikao cha juzi, kilihusisha viongozi saba na wadau kadhaa wakiwamo Friends of Simba, ikiwa ni ishara kuwa kwa sasa ni wamoja.
“Kuhusu suala la kocha, fanya subira kwanza, maana hapa nilipo bado tunaendelea na kikao, sijui kitaisha saa ngapi, isipokuwa mambo yanaenda vizuri,” alisema mmoja wa viongozi wa klabu hiyo.
Alisema kuna kila dalili kuwa, wajumbe wataafiki kutafutwa kocha wa kigeni kutoka nchi mojawapo barani Afrika kwani wa Ulaya gharama ni kubwa.
Tangu kuachwa solemba na Nielsen, Simba imekuwa chini ya Kocha Msaidizi, Madaraka Bendera, aliyeiwezesha kutinga hatua nya Sita Bora ya Ligi Ndogo.
Ikumbukwe, Nielsen alitua Simba akirithi mikoba iliyokuwa imeachwa na Mbrazil, mwingine, Neider do Santos, ambaye baada ya kwenda kwao kwa mapumziko, aligoma kurudi.