RAIS Jakaya Kikwete, amesema atalazimika kuchukua maamuzi mazito ambayo hayatawapendeza wengi ili kuinusuru bandari ya Kigoma.
Kikwete alitoa kauli hiyo juzi mara baada ya kuitembelea bandari hiyo na kukagua shughuli mbalimbali zinazofanywa bandarini hapo, na Mamlaka ya Bandari (TPA) na Shirika la Reli (TRC) kabla ya kuzindua boti ya kisasa ya doria inayomilikiwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).
“Taarifa nilizozisikia kuhusu bandari, si nzuri hata kidogo, kina cha maji kinaendelea kupungua, ni lazima tufanye utaratibu wa kuinusuru bandari ya Kigoma na maamuzi yale yatakuwa magumu na yatawaudhi watu wengi, lakini lazima tufanye uamuzi,” alisema rais.
Alisema serikali haiwezi kuiacha bandari hiyo itoweke kwa kuogopa kuwaudhi watu fulani, ambao hata hivyo hakuwataja, aliowaelezea kuwa ndiyo watakaokuwa wa kwanza kulaumu.
Rais alisema hatua yoyote ya kuruhusu kufa kwa bandari hiyo, itakuwa na maana ya kuruhusu kifo cha kiuchumi cha Kigoma, ambayo uchumi wake unaitegemea sana.
Alisema kuwa kwa kasi inayokwenda hivi sasa ya ushukaji wa kina cha maji katika bandari hiyo, ni wazi kuwa katika miaka mitano ijayo, hakutakuwa na bandari hiyo.
“Tayari nimekwisha mdokeza Waziri wa Miundombinu, Andrew Chenge nini nataka kifanyike, lakini pia ninaitaka Halmashauri ya Kigoma Ujiji nayo kukaa na kupanga nini watafanya kuinusuru bandari hii na waniletee taarifa, na nitakaa nao na kuwasikiliza madiwani na wabunge kabla sijaondoka hapa.”
Aliwataka madiwani na wabunge wa mkoa huo kutoa ushirikiao katika kuinusuru bandari hiyo iliyojengwa kati ya mwaka 1922 na 1927.
“Kilio kina mwenyewe na Halmashauri ya Kigoma/Ujiji ndio inayotakiwa ianze kulia kuhusu hatari ya kutoweka kwa bandari hii, wasipolia wao hakuna mwingine atakayelia kwa niaba yao, lazima mchukue tahadhari ya kuinusuru bandari hii,” alisema.
Akitoa taarifa fupi ya utendaji kazi wa bandari hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Ephraim Ngoza Mgawe, alisema ufanisi wa bandari hiyo umekuwa ukishuka mwaka hadi mwaka kutokana na matatizo kadhaa yanayoikabili.
Aliyataja baadhi ya matatizo hayo kuwa ni kuendelea kupungua kwa kasi kwa kina cha maji katika bandari hiyo kunakosababishwa na uchafuzi wa mazingira kwa baadhi ya watu kujenga katika vilima vilivyo karibu na bandari hiyo, na hivyo kufanya mchanga na udongo kuporomoka wakati wa mvua na kuingia ziwani.
Alisema sababu nyingine ni miundombinu ya maji taka kutoka katika mji huo kumwaga maji machafu katika mlango wa bandari, na hivyo kusababisha uchafu na mchanga kujaa katika eneo hilo na kufanya kina cha maji kupungua.
Alisema kina cha maji katika bandari hiyo kimeshuka kutoka meta sita hadi 1.83 na kwamba katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, kuanzia 2000 hadi 2006, kina cha maji kilipungua kwa meta mbili.
Hali hiyo imezifanya meli kubwa kushindwa kutia nanga katika gati ya bandari hiyo na kutia nanga mbali kidogo, na hata hizo zinazotia nanga zinatakiwa kusaidiwa na meli nyingine ili kuziweka sawa.
Mgawe alizitaja baadhi ya hatua ambazo mamlaka zinachukua kupambana na kujaa kwa mchanga na tope katika bandari hiyo kuwa ni pamoja na kuchimbua ili kuondoa mchanga, na pia inafanya mazungumzo na uongozi wa halmashauri ili ibadili mwelekeo wa miundombinu ya maji machafu ili yamwagwe mbali zaidi na eneo la bandari.
Akiwa bandarini hapo, Rais Kikwete alionyeshwa mtambo wa kunyanyua mizigo ambayo ilifungwa katika bandari hiyo mwaka 1922 na ambayo bado inafanya kazi.
Bandari hiyo ya Kigoma ni kiungo muhimu cha biashara na usafirishaji wa bidhaa na abiria kati ya nchi za Tanzania, Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
Awali, Mkurugenzi Mkuu wa TRC, Mboma alimweleza Rais kwamba ingawa reli hiyo bado inaendelea kusafirisha bidhaa mbalimbali kwenda nchi jirani, lakini tani za mizigo zinaendelea kushuka kutokana na ukosefu wa mabehewa ya kutosha na uchakavu wa miundombinu.