SERIKALI ya Tanzania imetishia kusitisha mpango wake wa kuwapa mafunzo wanajeshi 1,000 wa Somalia, iwapo waasi wa nchi hiyo hawatawaachia huru watu 24 waliowateka kutoka katika meli mbili za Korea ya Kusini.
Msimamo huo wa serikali ulitolewa jana jijini Dar es Salaam na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, alipokuwa akitoa taarifa ya ziara ya siku saba aliyoifanya nchini Japan na Korea ya Kusini.
Alisema akiwa Korea Kusini, alipewa taarifa za kutekwa kwa meli mbili za nchi hiyo kwenye mji wa Mombasa, Kenya. Meli hizo zimesajiliwa Zanzibar.
Membe alisema kama nchi iliyo katika ukanda ambao meli hizo zilitekwa, Tanzania ina wajibu wa kujihusisha na utekaji huo na kuhakikisha kuwa mateka hao wanaachiwa salama bila masharti yoyote.
“Kwa namna moja ama nyingine tunahusika na utekwaji huo, si kwa sababu tu meli hizo zimesajiliwa nchini Tanzania, bali sisi pia tupo kwenye ukanda wa Afrika Mashariki, zilipotekwa meli husika.
“Ikumbukwe kwamba tupo kwenye utaratibu wa kuwapa mafunzo ya kijeshi askari wa Kisomali wapatao 1,000, sasa kama wamewateka watu hatuwezi kuendelea na programu hiyo.
“Tunaiomba Serikali ya Somalia kuwasihi maharamia hao ili wawaachie mateka hao kwa kuwa tutakuwa tunawafundisha maharamia,” alisema Membe.
Habari zilizopatikana zinaeleza kuwa maharamia hao wanataka wapatiwe fedha na nchi ambazo raia wake wametekwa, kama sharti la kuwaachia raia hao.
Membe aliwataja raia wa nchi mbalimbali waliokuwemo kwenye meli hizo kuwa ni Wachina 10, Wakorea Kusini wanne, raia wa India watatu na Waindonesia wanne.
Alisema taarifa zilizopo zinaonyesha kuwa mateka hao wapo salama na wamehifadhiwa kusini mwa Somalia, huku maharamia hao wakishinikiza kulipwa fedha na nchi husika.
“Tumesikitishwa na kitendo hicho, tunaiomba Serikali ya Somalia kuwashawishi maharamia hao wawaachie huru watu wasio na hatia.
“Ahadi ya kuwapa mafunzo ya kijeshi raia wa Somalia ilikuwa ni mchango wa Tanzania kwa nchi hiyo lakini tunapata wasiwasi tusije kuwafundisha maharamia mbinu za kijeshi,” alisisitiza Membe.
Utekaji huo ulitokea kwenye pwani ya Mombasa Mei 15 mwaka huu, majira ya saa 5 asubuhi wakati meli hizo zikitokea Mombasa kuelekea Yemen.