WAZIRI Mkuu wa China , Wen Jiabao, amesema serikali yake itaendelea kutoa misaada kwa Tanzania baada ya kuridhishwa na kasi ya maendeleo yanayonekana hivi sasa nchini.
Waziri Jiabao alitoa kauli hiyo mwishoni mwa wiki, Ikulu Dar es Salaam mara baada ya serikali yake kutiliana sahihi mkataba wa ushirikiano na Tanzania katika nyanja mbalimbali zikiwamo za biashara, dawa za tiba ya malaria na sekata ya kilimo.
“Hatua ya maendeleo iliyofikiwa na Tanzania inapaswa kuungwa mkono, kwa maana tayari imeonyesha njia za wazi kupambana na umasikini,” alisema Jiabao.
Alisema kwa vile China na Tanzania zimekuwa na urafiki wa muda mrefu, itaendelea kutumia uwezo ambao imefikia sasa katika ulimwengu wa biashara, ili kuhakikisha Watanzania nao wanafaidi.
Waziri Mkuu Edward Lowassa, katika mazungumzo yake na mgeni wake ofisini kwake ,aliishukuru Serikali ya China kwa kuwa mstari wa mbele kutoa misaada yake hasa nchi ilipokuwa na uhaba wa chakula kutokana na ukame.
Katika ziara yake hiyo, Jiabao alitembelea makaburi ya Majohe yaliyoko Gongo la Mboto ili kuweka mashada ya maua kwa raia wa nchi hiyo waliokufa katika miaka ya sabini wakati wa kazi ya kujenga reli ya Tanzania na Zambia (TAZARA).
Waziri Jiabao alikuwa nchini kwa ziara ya siku mbili, na aliondoka juzi kuelekea nchini Uganda . Hii ni mara ya kwanza kwa Waziri Mkuu wa China kutembelea nchi 10 barani Afrika