ALIYEKUWA Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Ukiwaona Ditopile Mzuzuri, amewasilisha ombi katika Mahakama Kuu, akiiomba ifanye marekebisho ya moja ya masharti ya dhamana, katika kesi yake ya mauaji bila kukusudia.
Katika ombi hilo, Ditopile, anaiomba mahakama irekebishe sharti linalomtaka asitoke nje ya Mkoa wa Dar es Salaam bila kutoa taarifa kwa Msajili wa Mahakama hiyo.
Vyanzo vya habari kutoka ndani ya Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, viliiambia Tanzania Daima jana kuwa, ombi hilo namba 21 la mwaka 2007, liliwasilishwa na mawakili wanaomtetea Ditopile, mwishoni mwa mwezi uliopita. Hata hivyo, bado mahakama hiyo haijapanga tarehe ya kusikiliza ombi hilo.
Kwa mujibu wa vyanzo hivyo, Ditopile anaiomba mahakama ifanyie marekebisho sharti hilo lililowekwa na Jaji Augustine Mwarija, Machi 8, mwaka huu, wakati akisikiliza shitaka la msingi namba 13 la mwaka 2007, lililowasilishwa mahakamani hapo kutoka katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.
Katika ombi hilo, Ditopile ameitaka mahakama ifikirie hali yake ya sasa, na kubaini kuwa, sharti hilo linamkwamisha kuendesha maisha yake.
Anaeleza katika ombi hilo kuwa, hivi sasa yeye si mwajiriwa wa serikali, na amekuwa akitegemea shughuli zake binafsi kwa ajili ya kuendesha maisha.
Anabainisha katika ombi hilo kuwa, shughuli zake nyingi zipo katika maeneo ya Mkoa wa Pwani katika wilaya za Kisarawe na Kibaha.
Kwa maana hiyo, Ditopile anaiomba mahakama ilegeze sharti hilo ili aruhusiwe kwenda mkoani Pwani bila kuwa na ulazima wa kutoa taarifa, kwa kuwa kule ndiko kwenye shughuli zake za kilimo ambazo kwa sasa zinamsaidia kujikimu.
Mmoja wa mawakili anayemtetea, Dk. Ringo Tenga, akizungumza na gazeti hili ofisini kwake jana, alithibitisha kuwa ni kweli wamewasilisha ombi hilo mwishoni mwa Aprili mwaka huu.
Dk. Tenga alisema kuwa wamelazimika kuwasilisha ombi hilo kwa kuzingatia kuwa mteja wao kwa sasa si mfanyakazi wa serikali na amekuwa akitegemea shughuli zake za kilimo zilizopo mkoani Pwani kujikimu.
“Ni kweli tumewasilisha ombi hilo ingawa bado halijapangiwa tarehe ya kusikilizwa, na kisheria mteja wetu ana haki ya kuwasilisha ombi la aina hiyo… hivyo hapa tunachokisuburi ni mahakama ipange tarehe ya kusikiliza ombi hilo,” alisema wakili huyo.
Katika kesi ya msingi namba 13 ya mwaka 2007, Ditopile anatuhumiwa kumuua dereva wa daladala Hassan Mbonde, Novemba 2006 majira ya saa 1:40 usiku, eneo la Lugalo, Dar es Salaam.
Machi 8 mwaka huu, Mahakama Kuu ilimpatia Ditopile ambaye alikuwa amekaa rumande katika Gereza la Keko kwa takriban miezi minne na nusu dhamana.
Kuachiwa kwa Ditopile kwa dhamana kuliandamana na vitendo kadhaa zikiwemo vurugu zilizoanzishwa na wanaoaminika kuwa ni jamaa na ndugu zake ambao waliwashambulia waandishi wa habari.
Katika vurugu hizo, waandishi kadhaa walijeruhiwa na wengine kuharibikiwa vitendea kazi vyao, zikiwamo kamera.