WAKATI kukiwa na kelele kuhusu mwenendo usioridhisha wa matumizi ya fedha za umma na baadhi ya wizara kukabiliwa na tuhuma za utendaji mbaya wa kazi, Rais Jakaya Kikwete, amefanya mabadiliko madogo mazito ya watendaji wakuu serikalini.
Miongoni mwa maafisa wa juu walioguswa na mabadiliko hayo, ni Mhasibu Mkuu wa Serikali, Blandina Nyoni na makatibu wakuu wawili wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Hilda Gondwe na mwenzake wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Salehe Pamba.
Taarifa ya Ikulu iliyosainiwa na Katibu Mkuu Kiongozi, Philemon Luhanjo ilisema wakati Nyoni ameteuliwa kuwa Katibu Mkuu katika Wizara ya Maliasili na Utalii, wenzake wawili, Gondwe na Pamba wanasubiri kupangiwa kazi nyingine.
Katika mabadiliko hayo yaliyoanza juzi, Mei 17, Rais Kikwete, pia amefanya uteuzi wa makatibu wakuu watatu wapya kuchukua nafasi za hao wawili na mmoja ambaye amestaafu.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Ruth Mollel, aliyekuwa Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, amehamishiwa Ofisi ya Makamu wa Rais, akichukua nafasi iliyoachwa wazi na Abubakar Rajabu, aliyestaafu hivi karibuni.
Katika uteuzi wa makatibu wakuu wapya, Rais Kikwete amemteua George Yambesi kuwa Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma. Kabla ya uteuzi huo Yambesi alikuwa Naibu Katibu Mkuu kwenye ofisi hiyo hiyo.
Aidha, Rais Kikwete amemteua aliyewahi kuwa Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam, Wilson Mukama, kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii. Kabla ya uteuzi huo, Mukama alikuwa Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu, TAMISEMI.
Hata hivyo, taarifa hiyo haikueleza ni nani atachukua nafasi ya Mhasibu Mkuu wa Serikali iliyoachwa wazi na Nyoni.
Hii sasa ni mara ya pili kwa Rais Kikwete kufanya mabadiliko ya makatibu wakuu, baada ya kuchukua hatua kama hiyo mwishoni mwa mwaka jana.