MWENYEKITI wa Chama cha Tanzania Labour (TLP), Agustine Mrema, amesema amepanga kuunda tume itakayomhoji Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Dar es Salaam (UDSM), Profesa Rwekaza Mukandala, kuhusiana na tuhuma za kukivuruga chuo hicho.
Akizungumza na Tanzania Daima jana ofisini kwake jijini Dar es Salaam, Mrema alisema kuwa matatizo yaliyokikumba chuo hicho siku chache baada ya kukabidhiwa madaraka ya kukiongoza, yamedhihirisha kuwa Mukandala hana uwezo wa kukiongoza chuo kikuu.
Akiizungumzia tume hiyo, alisema kuwa yeye ndiye atakuwa mwenyekiti wake, na watamfuata kumhoiji Mukandala kwa kina kuhusiana na sakata la kusimamishwa kwa wanafunzi na migomo chuoni hapo.
Alisema baada ya kumaliza kumhoji Profesa Mukandala, tume yake itatoa taarifa kwa umma kuhusiana na mahojiano hayo.
Mrema alimtaka Mukandala kuendesha chuo kikuu kama taasisi ya elimu ya juu ambayo inapania kutoa viongozi wa baadaye wa taifa.
Mrema alidai kuwa mgogoro unaoendelea hivi sasa UDSM umekuzwa bila sababu za msingi na uongozi wa chuo na serikali kwani kiasi cha fedha ambacho wanafunzi walikuwa wanakihitaji ni kidogo mno ukilinganisha na hasara ambayo taifa limepata kutokana na kusimamishwa kwa masomo chuoni hapo kwa takriban mwezi mmoja.
Wanafunzi hao waligoma wakiitaka serikali iwapatie ufadhili wa gharama za masomo kwa asilimia 100, badala ya asilimia 60 inayoitoa hivi sasa kupitia Bodi ya Mikopo kwa Wanafunzi wa Elimu ya Juu.