MWANDISHI wa habari wa Tanzania Daima, Anna Makange, aliyejeruhiwa na askari wa kikosi cha kutuliza ghasia (FFU), hivi karibuni mkoani Tanga, hali yake imezidi kuwa mbaya kutokana na kipigo hicho.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa njia ya simu jana, Makange alisema kuwa hivi sasa anasumbuliwa na maumivu ya mgongo na miguu kufa ganzi mara kwa mara.
Alisema mwanzoni mwa wiki hii, alilazwa katika Hospitali ya Bombo alikokuwa akipatiwa matibabu na ameruhusiwa juzi, huku akishauriwa muda mwingi alale chini kwa muda wa wiki mbili.
“Wameniambia uti wa mgongo kama una ufa, hivyo nilale chini kwa wiki mbili kisha nirudi hospitali kuangalia kama nitapata nafuu na kurudi katika hali ya kawaida, ikishindikana itabidi wanihamishie Hospitali ya Muhimbili.
“Pia kuanzia kwenye magoti mpaka chini nilikuwa nahisi ganzi, lakini baada ya kupewa dawa ya kuchua, hivi sasa ganzi imebaki kwenye nyayo,” alisema Makange ambaye kutokana na hali hiyo hawezi kutembea sawasawa.
Askari hao wa FFU, walimpiga mwandishi huyo wa habari Aprili 12 mwaka huu, wakati akitekeleza wajibu wake wa uandishi wa habari.
Askari hao walikuwa wakienda eneo la Pongwe kuangalia hali ya usalama baada ya wananchi kuziba njia kwa muda, wakishinikiza serikali ya mkoa kujenga matuta barabarani katika eneo hilo.
Wananchi hao, walichukua hatua hiyo baada ya mtoto mmoja wa miaka sita aliyetambulika kwa jina la Kuluthumu Athumani, kufariki dunia baada ya kugongwa na gari.
Awali, kwa mujibu wa maelezo yaliyotolewa na Makange, askari hao walionekana wakimnyemelea baada ya kuona akizungumza na familia ya mtoto aliyekufa baada ya kugongwa na gari.
Makange alisema baada ya kuzungumza na familia hiyo, wakati anaondoka, askari hao walimfuata na kuanza kumpiga, huku wakimshutumu kuwa amekwenda kuanzisha vurugu katika eneo hilo.
Habari zaidi kutoka Tanga zinaeleza kuwa, katika siku za hivi karibuni na hasa baada ya afya ya Makange kutokuwa nzuri, zimekuwapo juhudi za chinichini za makusudi za kulifanya tukio hilo la mwandishi kupigwa kutolihusisha jeshi hilo katika mazingira yanayoonyesha nia ya kuficha ukweli.
Hili ni tukio la pili la mwaka huu kwa waandishi kupigwa wakiwa kazini, baada ya lile la ndugu na jamaa wa aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Ukiwaona Ditopile Mzuzuri kufanya hivyo siku mwanasiasa huyo alipopewa dhamana.