WAKAZI wa Arusha wametakiwa kutumia mbwa wa kisasa katika masuala ya ulinzi wa majumbani na kuondoa dhana kuwa kumiliki silaha kuwa ndiyo suluhisho la kukabiliana na vitendo vya ujambazi.
Wito huo ulitolewa jana na kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Wenceslaus Magoha, wakati akizindua rasmi mradi wa uzalishaji mbwa wa kisasa ulioanzishwa na mwanasheria wa kujitegemea, Hubert Makange, wa mjini hapa.
Kamanda Magoha alisema kuwa hivi sasa wakazi wengi wa Arusha wanahangaika kupata vibali vya kumiliki silaha vinavyochukua muda mrefu kupatikana kutokana na taratibu za utoaji vibali kuwa nyingi.
Aliwataka wabadili mwelekeo na kujenga utamaduni wa kuwatumia mbwa wa kisasa waliofundishwa kazi ya ulinzi.
Aliongeza kuwa katika nchi nyingi zinazoendelea na zilizoendelea, wananchi wengi hutumia mbwa kwa ulinzi kwa kuwa matuimizi ya silaha yana taratibu ambazo mtumiaji asipozifuata sawasawa, anaweza kujiingiza katika matatizo.
Wakili Makange alisema aliuanzisha mradi huo kama moja ya jitihada zake za kusaidia jamii katika masuala ya ulinzi kutokana na kushamiri kwa vitendo vya ujambazi.
Alisema amepata mbegu ya mbwa hao kutoka katika nchi mbalimbali ikiwamo Afrika Kusini. Huko mbwa hao wanapata mafunzo kutoka kwa wataalamu.
Aidha, alilikabidhi Jeshi la Polisi mkoani humu mbwa mmoja jike, mwenye thamani ya dola 500, aliyekwishapata mafunzo kamili ya ulinzi, ili kuchangia jitihada za jeshi hilo katika kukabiliana na wahalifu.