KUNDI la muziki wa asili la Machozi limeshindwa kuthibitisha ushiriki katika sherehe za Uhuru wa Zambia zitakazofanyika Mei 23, mwaka huu, jijini Lusaka.
Akizungumza juzi jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Shirikisho la Wasanii Tanzania (SHIWATA), Twalib Kassim, alisema kundi hilo litashindwa kushiriki sherehe hizo kutokana na wasanii wake kutokuwa na hati za kusafiria.
Kassim alisema licha ya wasanii hao kupewa muda wa kuandaa paspoti hizo, hadi Aprili 27 walikuwa bado hawajamilisha taratibu hizo.
Mwenyekiti huyo alisema baada ya kundi hilo kushindwa kukamilisha taratibu hizo, SHIWATA imelipendekeza kundi la Mandela Theatre kuchukua nafasi hiyo baada ya kukamilisha taratibu hizo.
Aidha, Kassim alisema mbali ya Machozi, pia kundi la ngoma la JKT nalo limeshindwa kuthibitisha kushiriki sherehe hizo kutokana na tatizo kama la Machozi.
Kassim alisema kutokana na tatizo hilo, JKT hawatashiriki katika sherehe hizo na hakuna kundi lolote lililopewa nafasi hiyo.
Katika sherehe hizo za Uhuru wa Zambia, kundi la Mandela litashiriki katika upande wa muziki wa asili na Jeshi la Ulinzi la Wananchi Tanzania (JWTZ) litashiriki katika upande wa sarakasi.
Kassim alisema kukosa huko kwa hati za kusafiria kwa makundi ya JKT na Machozi si kwamba ndiyo mwisho wa makundi hayo, bali wanayataka yajipange kwa safari nyingine zitakazojitokeza.