SERIKALI imetoa taarifa bungeni, ikitetea uamuzi wa Rais Jakaya Kikwete kumteua Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam , Yusufu Makamba, kuwa mbunge katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania .
Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Johnson Mwanyika, jana alitoa taarifa hiyo ya utetezi kutokana na maelezo ya Mbunge wa Bariadi Mashariki, John Cheyo (UDP), aliyeonyesha wasiwasi kuhusu uteuzi wa Makamba.
Mwanyika alisema uteuzi wa Makamba kuwa mbunge umefanyika kwa mujibu wa masharti ya Ibara ya 66(1)(e) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania .
Alisema suala la kuwa au kutokuwa na sifa za kuweza kuteuliwa kuwa mbunge, limewekewa masharti katika Ibara ya 67 ya Katiba.
“Masharti aliyozungumzia Mheshimiwa Cheyo ni yale yaliyomo kwenye aya ya (g) ya Ibara Ndogo ya (2),” alisema.
Ibara hiyo inaeleza: “Mtu hatakuwa na sifa za kustahili kuchaguliwa au kuteuliwa kuwa mbunge:- (g) ikiwa mtu huyo ameshika madaraka ya ofisa mwandamizi katika utumishi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano isipokuwa madaraka ambayo Rais anaweza au anatakiwa kukabidhi kwa mbunge kwa mujibu wa katiba hii au sheria iliyotungwa na Bunge.”
Mwanyika alisema, ikiwa mtu ameshika madaraka kwa ngazi ya ofisa mwandamizi katika utumishi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano, na madaraka hayo ni ya aina ambayo yanaweza au yanastahili kukabidhiwa kwa mbunge, basi mtumishi huyo hapotezi sifa za kustahili kuchaguliwa au kuteuliwa kuwa mbunge.
Mwanyika alisema kwa mujibu wa katiba, Mkuu wa Mkoa ni kiongozi wa kisiasa katika Serikali ya Jamhuri ya Muungano, na si ofisa mwandamizi.
“Mtu anayeitwa kiongozi katika serikali anayetajwa, ni kama vile Rais, Waziri Mkuu, Waziri, Mkuu wa Mkoa na kadhalika.
“Watu hawa si maofisa waandamizi katika utumishi wa serikali kama walivyo makatibu wakuu au wakurugenzi.
“Ukuu wa mkoa ni madaraka ambayo Rais anaweza kukabidhi kwa mbunge. Kinyume chake pia, ni sahihi kwamba Rais anaweza kumteua mtu ambaye ni mbunge kushika madaraka ya Mkuu wa Mkoa.
“Kwa ofisa mwandamizi katika utumishi wa serikali, yeye hana sifa za kuteuliwa kuwa mbunge.
“Rais anapomteua Mkuu wa Mkoa kuwa mbunge, uteuzi huo ni wa kisiasa, hivyo haukiuki masharti ya Ibara ya 67(2)(g) ya katiba, kwani ukuu wa mkoa ni ofisi ya kisiasa, na si utumishi wa serikali,” alihitimisha Mwanyika.
Wabunge wengine ambao ni wakuu wa mikoa ni Mohammed Abdulaziz (Tanga), Monica Mbega (Ruvuma), William Lukuvi ( Dodoma ) na Dk. James Msekela (Mwanza).