KATIBU Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad, amesema ziara zinazofanywa na viongozi wa kitaifa nje ya nchi, zingekuwa na manufaa makubwa kwa nchi iwapo zingekuwa zinapangiliwa vizuri badala ya kufanywa picnic kama ilivyo sasa.
Alisema hivi sasa ziara hizo hazileti manufaa makubwa kwa taifa kwa sababu zinalenga zaidi katika kutekeleza malengo binafsi ya baadhi ya watu wanaopangwa kuwamo katika ziara hizo.
Akizungumza na gazeti hili nyumbani kwake Mtoni, mjini Unguja, siku chache kabla ya maadhimisho ya miaka 43 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, Maalim Seif alibainisha kuwa, baadhi ya viongozi huzitumia ziara za nje kama picnic.
Alisema kwamba ziara za viongozi nje ya nchi kama zitatumiwa vizuri upo uwezekano mkubwa wa kuleta maendeleo, na katika hilo Tanzania inaweza kujifunza katika nchi nyingi ambazo zimepiga hatua za kimaendeleo.
Katibu Mkuu huyo wa CUF alisema tatizo kubwa linaloikabili Tanzania hasa Zanzibar, ni viongozi kutowashirikisha watendaji katika ziara za nje na hivyo kushindwa kujifunza njia na mikakati bora ya uzalishaji wa kisasa.
Alisema kwamba ni jambo la kushangaza Zanzibar imezunguukwa na bahari, lakini imeshindwa kuwekeza katika uvuvi wa bahari kuu na viwanda.
Katibu Mkuu huyo alisema kwamba Taiwan imeweza kupiga hatua kubwa ya maendeleo kutoka na shughuli za ufugaji wa samaki wa maji baridi na baharini pamoja na uzalishaji wa maua.
“Viongozi wasitumie ziara ya nje kama picnic, waende katika mataifa yaliyopiga hatua kubwa kimaendeleo na baadaye warudi na ujuzi utakaosaidia kubadilisha hali ya mambo nchini,” alisema Hamad, ambaye pia ni Waziri Kiongozi mstaafu.
Aliyazungumza hayo siku chache tu baada ya yeye na mwenyekiti wa chama chake, Profesa Ibrahim Lipumba, kumaliza ziara ya ktakriban siku 10 nchini Taiwan.
Alieleza kwamba, Taiwan imeweza kupiga hatua kubwa ya maendeleo baada ya kuwekeza katika sekta ya elimu na kuimarisha misingi ya demokrasia.
Akitoa ufafanuzi kuhusu nafasi ya demokrasia katika ujenzi wa uchumi, Maalim Seif alibainisha kuwa, demokrasia ina nafasi kubwa katika kujenga serikali yenye kuwajibika kwa vile ndio uwanja pekee wa kukosolewa pale inapofanya vibaya.
Alieleza kwamba, Zanzibar ina mambo mengi ya kujifunza kutoka Taiwan, kwani nayo ni nchi ya kisiwa kama ilivyo Zanzibar na imepiga hatua kubwa kimaendeleo.
Akichambua utendaji wa viongozi waliopo madarakani, alisema kwamba mpango wa Zanzibar wa kuanzisha kilimo cha umwagiliaji ulioanzishwa na rais wa awamu ya nne, marehemu Mzee Idrisa Abdulwakil, ulioitwa MTAKULA, umeshindwa kuendelezwa Zanzibar kutokanana viongozi
Kung’ang’ania maofisini badala ya kwenda mashambani kusimamia utekelezaji.
Alisema kwamba hivi sasa wakulima na wavuvi wanakabiliwa na matatizo mbalimbali, lakini hawana mtu anayewasaidia kutatua kero zao kwa vile wataalamu wanabakia maofisini na viongozi wa kisiasa hawana utamaduni wa kwenda kusikiliza matatizo ya wakulima na wavuvi.
“Mimi nilipokuwa Waziri Kiongozi nilikuwa naenda mabondeni kuanzia asubuhi hadi jioni kuwasikiliza wakulima, kwa vile huwezi kuleta mabadiliko ya uzalishaji bila ya kusimamia,” alisema Hamad.
Alieleza kwamba nchi nyingi zilizopiga hatua zimewekeza katika sekta za viwanda kwa vile ndio njia pekee ya kuongeza ajira na pato la taifa.