*Mabasi ya mikoani, daladala zote ukaguliwa leo
*Usafi wa sare za makondakta nao kuangaliwa
Na Mwandishi Wetu MAELFU ya wakazi wa jiji la Dar es Salaam na vitongoji vyake, huenda leo wakakumbwa na shida kubwa ya usafiri baada ya Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (Sumatra) kuamua kufanya operesheni maalum ya kukamata daladala zinazokiuka utaratibu.
Meneja Mawasiliano wa Sumatra, David Mziray, ameliambia Mwananchi ofisini kwake jijini Dar es Salaam jana, kwamba maandalizi ya operesheni hiyo yamekamilika.
Mziray alisema operesheni hiyo maalum ya leo, itahusisha ukamataji wa makondakta na madereva wakorofi wa daladala, mabasi ya kubeba wanafunzi na mabasi ya mikoani yanayotoka au kuingia jijini Dar es Salaam.
Kwa upande wa daladala, operesheni hiyo itafanyika katika wilaya zote za jiji la Dar es Salaam na kwamba gari, madereva na makondakta watakaokamatwa, watapelekwa katika vituo vya polisi vitakavyopangwa.
Asilimia kubwa ya daladala zinazofanya kazi kati njia mbalimbali za jijini Dar es Salaam aidha zipo katika viwango visivyotakiwa au kuendesha huduma hiyo kwa abiria kwa ukiukwaji mkubwa wa sheria, hali ambayo inafanya kuwe na uwezekano mkubwa wa gari nyingi za aina hiyo kutokuwapo barabarani.
Tayari Sumatra imekwishawaarifu wamiliki wa daladala, mabasi ya mikoani na yale ya kubeba wanafunzi, wahakikishe madereva na makondakta wao wanafuata sheria za barabarani.
Mziray alisema miongoni mwa mambo yatakayohusika katika operesheni hiyo ni pamoja na ukaguzi wa leseni za usafirishaji kwa kuhakikisha daladala zinapita katika njia zilizopangwa na kupita barabarani na si pembeni.
Mziray alifafanua kwamba, kwa makusudi au kutofahamu, baadhi ya wasafirishaji wakiwemo wa mabasi yaendayo mikoani, huamua kutoa leseni ambazo ni za kughushi.
"Sumatra inawaagiza wasafirishaji ambao hawana uhakika na uhalali wa leseni zao, walipaswa kufika katika ofisi za mamlaka kwa ajili ya kufanya uhakiki wa uhalali wa leseni zao kabla zoezi kuanza," alisema Mziray.
Mziray alisema operesheni hiyo ambayo itaendelea kuanzia leo, itahusisha pia ukaguzi wa ubora wa magari, huduma na utekelezaji wa masharti ya leseni.
Katika operesheni hiyo, kila msafirishaji atapaswa kuwa na leseni hai na halali ya usafirishaji katika basi lake, ratiba ya njia kwa mabasi ya kwenda mikoani na gari lipakwe rangi ya njia ambako leseni imeelekeza (kwa daladala).
Mziray aliongeza kuwa madereva na makondakta watapaswa kuvaa sare safi na zenye muhuri unaoonyesha namba ya gari wanayohudumia na kuhakikisha abiria wanapanda na kushuka katika vituo vinavyostahili.
"Msafirishaji ambaye gari lake litakutwa na makosa yaliyotajwa hapo juu, atatozwa faini hapo hapo kulingana na kosa lenyewe," alionya.
Alisema wasifirishaji ambao watakutwa na leseni za kughushi watatozwa faini kwa kosa la kufanya biashara ya usafirishaji bila leseni na atashtakiwa mahakamani kwa kosa la kutumia leseni ya kughushi