KAMA kuna jambo baya kwa watu waliostaarabika, ambalo mara nyingi hushusha heshima ya mtu bila kujali wadhifa wake, ahadi za uongo au zisizotekelezeka.
Jambo hili haliishii kwa waliostaarabika tu, bali hata kwa watoto wadogo, ambao kama mzazi wao akizoea kuwadanganya kuwatimizia mahitaji yao au ahadi nyingine yoyote, watoto hao hupungukiwa na upendo kwa mzazi wao.
Tunatoa kauli hii kwa makusudi kabisa tukimaanisha ahadi za serikali yetu, lakini kauli yetu hii ina nia njema ya kuwakumbusha viongozi wetu kuwa ahadi nyingi wanazotoa bila kuzitekeleza zina madhara yake tena makubwa.
Tangu Serikali ya Awamu ya Nne ilipoingia madarakani, viongozi wake wakuu wamekuwa hawaishi tambo na majigambo.
Lakini kikubwa zaidi, wamekuwa mabingwa wa kutoa ahadi nyingi nzuri, ambazo utekelezaji wake umekuwa sawa na sifuri.
Ahadi zilizotolewa ni nyingi. Tunaamini kabisa kuwa serikali inajua imeahidi nini na imetekelezaje ahadi zake hizo, hivyo hatuna nia ya kuzirudia hapa, lakini tunashawishika kuikumbusha kuhusu ahadi yake kwa wanafunzi wa elimu ya juu kuwa hakuna mwanafunzi atakayekosa elimu ya juu kutokana na umaskini wa wazazi wake.
Ahadi hii ilitolewa na kiongozi mkuu wa nchi, Rais Jakaya Kikwete, wakati akizungumza na wasomi wetu katika Ukumbi wa Diamond Jubilee katika maadhimisho ya miaka 30 ya kuzaliwa kwa CCM.
Rais Kikwete alitoa ahadi hii Februari 5 na tangu alipoitoa miezi miwili imekwishakatika, lakini utekelezaji hauonekani, wasomi bado wanasota kutafuta asilimia 40 ya ada wanayopaswa kuchangia.
Tunatambua kuwa serikali ina mipango mingi, hivyo utekelezaji wa jambo hili unaweza kuchukua muda, hatuna tatizo na hilo kwa sababu huo ndio ukweli. Lakini kinachotutatiza ni ahadi iliyotolewa, tunajiuliza hii ahadi ilitolewa kimakosa au kwa sababu ya kuwapaka mafuta kwa mgongo wa chupa wasomi wetu.
Tunaamini kabisa kuwa serikali inao uwezo wa kutekeleza ahadi yake ya kuwalipia ada wanafunzi wa elimu ya juu kwa asilimia 100 bila uchumi wa nchi yetu kuyumba au kutetereka.
Imani yetu inatokana na taarifa za hivi karibuni kuwa kuna ubadhirifu wa kutisha katika matumuzi ya serikali unaofikia sh bilioni 900, lakini pamoja na ubadhirifu huo, bado mambo yanakwenda na serikali inaendelea kusonga mbele na mkakati wake wa kuhakikisha maisha bora kwa kila Mtanzania yanapatikana.
Tena imani yetu hiyo inatokana na jitihada za makusudi zilizofanywa na Rais Kikwete za kuhakikisha kuwa klabu maarufu ya mpira wa miguu ya Hispania ya Real Madrid inakuja nchini kufanya ziara ya siku chache huku ikitumia mabilioni ya shilingi.
Hapo ndipo tunapojiuliza, inashindikana nini kwa Rais Kikwete aliyefanikiwa kuwashawishi wafanyabiashara na wadau wengine wa soka pamoja na Watanzania kwa ujumla, kuchanga mabilioni ya shilingi kwa ajili ya kuileta timu ya Real Madrid, lakini ishindikane kuwahamasisha Watanzania na kuwaomba wahisani wa nje kuchangia kwa ajili ya ada ya wanafunzi wa elimu ya juu?
Hatuna nia ya kuingilia mpangilio wa kazi na vipambele vya kushughulikia mambo alivyojiwekea Rais wetu, lakini tuna haki ya kushangazwa na vitendo vyake kama mkuu wa taifa letu.
Tuna haki ya kushauri na kukosoa inapobidi na kwa mantiki hiyo tunahoji, serikali inashindwa nini kutekeleza ahadi zake, na kwa nini suala la wanafunzi wa elimu ya juu halipewi kipaumbele kama masuala mengine likiwamo la soka?