Na Daniel Mjema, Moshi
AJALI ya basi la kampuni ya Buffalo na lori iliyoua watu 22 na kujeruhi 18, imewazindua polisi mkoani hapa ambapo sasa wameanza kutumia kifaa maalumu kubaini magari (mabasi) yaliyo kwenye mwendo.
Matumizi ya kifaa hicho maalumu kinachoweza kugundua mwendo wa gari likiwa mbali, kilianza kutumika juzi baada ya kuletwa mkoani Kilimanjaro kutoka Makao Makuu ya Jeshi hilo, Jijini Dar es Salaa.
Kamanda wa Polisi mkoa Kilimanjaro, Lucas Ng'hoboko, alithibitisha jana kutumiwa kwa kifaa hicho na kusema kuwa kwa juzi pekee magari manne likiwemo basi la kampuni ya Meridian limenaswa.
Ng'hoboko alisema magari hayo yalipigwa faini ya papo kwa hapo na kwamba madereva watakaobainika kurudia kosa la mwendo kasi watashitakiwa mahakamani na kunyang'anywa leseni zao za udereva.
Hatua hiyo imekuja sambamba na Jeshi hilo kuwataka abiria wenye haraka na kushabikia mwendo kasi wa mabasi watumie usafiri wa ndege kama kweli wana haraka za kufika wanakokwenda.
Kauli hiyo ilitolewa juzi na Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani nchini, Kamishina Msaidizi Mwandamizi wa Polisi(SACP), James Kombe, baada ya kukutana kwa faragha na polisi wa usalama barabarani mkoa wa Kilimanjaro.
Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kikao hicho, bosi huyo wa Trafiki aliwataka abiria wenye haraka kusafiri siku moja kabla badala ya kusafiri siku hiyo hiyo na kutaka dereva aendeshe basi kwa mwendo kasi.
“kuna dhana ya kijinga sana unakuta abiria mmoja au wawili wanalalamikia mwendo kasi halafu wanatokea abiria wengine wanamkemea na kusema wana haraka…! Kama una haraka si upande ndege?” alisema na kuhoji Kombe.
Pia aliwataka abiria kuheshimu utaratibu wa kutopanda basi lililojaa maarufu na kusisitiza kwamba wakiona basi limejaa wapande basi lingine.
SACP Kombe alifafanua kuwa kikosi cha usalama barabarani kitaongezewa nguvu ili kukabiliana na madereva wakorofi wanaoendesha mabasi kwa mwendo kasi bila kujali maisha ya abiria wa mabasi hayo.
Naye Ally Sonda anaripoti kuwa; maiti mwingine wa ajali ya basi hilo,Leonard Christian Saria(48) atambuliwa juzi jioni hivyo kufanya jumla ya miili ya marehemu iliyotambuliwa kufikia 20 sasa.
Kamanda wa Polisi mkoa wa Kilimanjaro, Lucas Ng’hoboko alisema Saria alikuwa mkazi wa Msaranga Katika Manisapaa ya Moshi na kwamba alikuwa dereva.
Kwa mujibu wa Kamanda huyo maiti ambazo hadi jana jioni zilikuwa hazijatambuliwa na ndugu au jamaa zao ni mbili ikiwemo ya Mwanamke na Mwanume, wote watu wazima.
Kamanda Nghoboko amewataka wananchi kuendelea kufika kwenye chumba cha maiti Hospitali ya Mawenzi kuitambua miili hiyo.
Alisema hali za majeruhi wa ajali hiyo, akiwemo dereva wa basi la Bufallo zinaendelea vizuri kwenye Hospitali za Mawenzi na KCMC ambako wamelazwa kwa matibabu.
Na Omary Magongo, anaripoti toka Arusha, kuwa Chuo Kikuu cha Arusha (UoA) ni miongoni mwa
taasisi ziliathiriwa na tukio hilo baada ya mwanafunzi wao mmoja kufariki dunia katika ajali hiyo.
Akitoa taarifa rasmi ya kifo hicho kwa wanafunzi jana, Mkuu wa Kitivo cha Biashara na Uhasibu chuoni hapo, Cosmas Nyarusanda, alimtaja mwanafunzi
huyo kuwa ni Benedict Maufa aliyekuwa mwaka wa pili katika kitivo hicho.
Nyarusanda alisema mwanafunzi huyo aliyekuwa anasoma masomo ya jioni katika tawi la chuo hicho la Arusha mjini, mwili wake umehifadhiwa katika Hospitali ya Rufaa ya KCMC na mipango ya kuusafirisha kwenda kwao Ukerewe kwa mazishi inafanywa.