SAKATA la mgomo wa wanafunzi wa vyuo vikuu nchini, limechukua sura mpya siku moja baada ya Baraza la Uongozi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kuwasimamisha masomo wanafunzi hao kwa muda usiojulikana.
Sasa, wanasiasa wameingia katika suala hilo, wakiwaunga mkono wanafunzi hao waliogoma na kuipa serikali siku 21 kuwarejesha shuleni haraka.
Wakizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, viongozi wa vyama vitatu vya upinzani, waliitaka serikali kuhakikisha inawapa wanafunzi hao ufadhili wa asilimia 100 wa masomo.
Iwapo serikali itashindwa kufanya hivyo katika kipindi cha siku 21, viongozi hao walitishia kuchukua kile walichokiita, hatua za kisiasa na kisheria.
Tamko hilo limetolewa kwa pamoja na vyama vya NCCR-Mageuzi, Chama cha Wananchi (CUF) na Chama cha Tanzania Labour (TLP), kupitia mkutano wao na waandishi wa habari, uliofanyika jana kwenye ofisi za makao makuu ya NCCR, jijini Dar es Salaam.
Tamko hilo la wenyeviti wa taifa wa vyama hivyo, lilisomwa na James Mbatia ambaye pia alimwakilisha, Mwenyekiti wa TLP, Augustine Mrema wakati, Profesa Ibrahim Lipumba wa CUF aliwakilishwa na Naibu Katibu Mkuu wake, Wilfred Lwakatare.
Akisoma tamko hilo, Mbatia ambaye naye alipata kufukuzwa moja kwa moja Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam kwa sababu ya mgomo, alisema kuwa, wakiwa Watanzania wanaipa serikali siku 21 iwarejeshe wanafunzi hao masomoni bila masharti na itekeleze madai yao yote mara moja.
Alisema kuwa, hatua ya kisiasa ndio watakayoitumia zaidi kwa kuhamasisha wananchi kote nchini kugoma na kuandamana ili serikali itambue kuwa inaendesha nchi kwa shinikizo na si kwa ridhaa ya wananchi.
“Tutawahamasisha wananchi nchini kote waunge mkono ili haki zao zisichezewe na wachache kwa kuwa elimu ni haki ya msingi na kikatiba na ndio uhai wa nchi.
“Kinachoendelea hapa nchini ni kitu cha kusikitisha sana kwa kuwa ni wanafunzi hawa hawa ambao wengi wao walishindwa kulipa karo ya sh 70,000 wakiwa shule za sekondari, watapata wapi sh 500,000 sasa, wakati wanatoka katika familia zilizo katikati ya lindi la umaskini?” alihoji Mbatia.
Alisema kitendo hicho cha wanafunzi kugoma kinaonyesha wazi kuchoka kwao kupelekwa kama kondoo kwa kudanganywa na ubwabwa, soda, fulana na kapelo zenye rangi ya kijani na tatizo la maprofesa kujikomba kwa wanasiasa hali inayofanya taaluma kuwa siasa.
Aidha, kwa niaba ya viongozi wenzake, Mbatia alimuomba Rais Jakaya Kikwete atimize ahadi yake ambayo aliitoa wakati akiwapa wanafunzi wa vyuo vikuu kadi za UVCCM, katika Ukumbi wa Diamond Jubilee, Februari mwaka huu.
Alimtaka Kikwete aache kile alichokiita usanii na ujanja ujanja katika kuongoza nchi.
Alisema kitendo cha kufukuza wanafunzi hao kinatisha kwa kuwa rais aliwaahidi wanafunzi hao wakati alipowapa kadi za kujiunga na UVCCM kuwa, hakuna mwanafunzi kutoka familia maskini ambaye atafukuzwa chuo kwa kushindwa kulipa asilimia 40.
“Lakini cha ajabu, kama si kichekesho, wanafunzi hao wamefanyiwa kitendo cha kinyama cha kupewa saa moja kutoonekana eneo la chuo... waende wapi usiku huo?” alihoji.
Akinukuu taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali, alisema serikali kwa muda mfupi tu imeweza kutumia kiasi cha sh bilioni 978 kwa ubadhirifu na kushindwa kuwapa wanafunzi fedha wanazodai ambazo hazifiki hata sh bilioni 50.
Alisema serikali inakiuka katiba kwa kuwa suala ambalo wanataka wanafunzi hao si la hisani, bali ni la lazima kwa kuwa tamko la ulimwengu la haki za binadamu, linasema kila mtu ana haki ya kupata elimu.
“Kwa hiyo, kitendo cha kuwafukuza wanafunzi hao, kinaonyesha kuwa serikali haipo makini katika kupanga na kuchagua maamuzi na hicho ni kifo cha taifa,” aliongeza na kusisitiza kuwa, kigezo kikubwa cha kupima utaifa ni elimu.
Aliongeza kuwa, kufungwa kwa chuo kikuu kunafundisha kuwa baadhi ya wahadhiri waliokabidhiwa kuongoza vyuo vikuu nao wamechoka kifikra, na wameridhia kutokana na hasira yao inayotokana na mishahara midogo ambayo wanapewa.
Naye mwanasheria wa siku nyingi aliyepata kuwa mhadhiri wa Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam, Dk. Sengondo Mvungi, alisema wanafunzi hao hawakutakiwa kufukuzwa kwa kuwa sheria inasema kuwa mwanafunzi atafukuzwa iwapo tu, atagoma, kukataa kuzungumza na kufanya uharibifu wa mali.
“Lakini wanafunzi hao walikuwa tayari kuzungumza, hivyo walipaswa kusikilizwa… kugoma ni haki yao na kitendo cha wanafunzi hao kugoma kimeonyesha ni jinsi gani walivyo wasomi, kwani msomi yeyote ambaye anafundishwa na mhadhiri makini, hawezi kupelekeshwa kama kondoo kwa kukubali kila kitu,” alisema Dk. Mvungi.
Dk. Mvungi ambaye ni mwanasheria wa NCCR-Mageuzi, alisema iwapo wanafunzi hao wangekaa na kukubaliana na mambo wanayotendewa, wasingekuwa na sifa ya usomi.
Hata hivyo, alisema kilichotakiwa ni watawala kufikiria mara mbili juu ya mgomo huo na si kuwafukuza kwani hicho ni kitendo cha aibu ambacho hata yeye kinamfanya aone aibu kufundisha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM).