HOFU imetanda miongoni mwa mawaziri baada ya Rais Jakaya Kikwete kuitisha mkutano wa dharua leo kwa lengo la kujadili ubadhirifu wa fedha, uliobainishwa katika ripoti ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) ya mwaka 2005/2006.
Mbali ya mawaziri na manaibu wao, Rais Kikwete katika mkutano huo, pia atakutana na makatibu wakuu wa wizara na manaibu wao, wakuu wa mikoa, makatibu tawala wa mikoa, wahasibu wakuu na wahasibu wa ndani.
Tayari Rais Kikwete yuko mjini hapa na mkutano wa leo unafanyika ikiwa ni siku tatu tangu alipokutana na baraza lake la mawaziri kujadili hatua za kuchukua dhidi ya waliohusika na ubadhirifu wa fedha za serikali kama ilivyobainishwa katika ripoti ya CAG.
Baadhi ya mawaziri, hasa wa wizara zilizohusika na matumizi mabaya ya fedha na ubadhirifu, tangu kutolewa kwa ripoti hiyo, hawaonekani bungeni na badala yake wamekuwa na vikao vya dharura na manaibu, makatibu na manaibu wao pamoja na maofisa wengine ili kujipanga kukabiliana na hoja za Rais Kikwete katika mkutano huo.
Viongozi hao ambao kwa siku mbili sasa wameona viti vya bungeni vichungu, wamekuwa wakiongoza vikao hivyo nje ya Bunge katika baadhi ya hoteli kubwa mjini hapa.
Katika ripoti hiyo ya CAG, inaonyesha kuwa wizara 27 na wakala zao sawa na asilimia 39, zilipewa hati chafu zinazoonyesha kuwapo kwa ubadhirifu wa fedha.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, baadhi ya wizara zinazoongoza kuwa na matumizi mabaya na hivyo kupewa hati chafu ni pamoja na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Ofisi ya Waziri Mkuu na Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa.
Zinafuatiwa na Wizara ya Viwanda, Biashara na Masoko, Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Wizara ya Maji, Mambo ya Ndani, Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Wizara ya Maendeleo ya Jamii Jinsia na Watoto na Wizara ya Nishati na Madini.
Mbali ya taarifa ya CAG, taarifa nyingine ya Benki Kuu (BoT) inaonyesha kuwa, hadi Februari mwaka huu, serikali imeshatumia sh bilioni 978.8 zaidi ya bajeti yake.
Kikao kingine kama hicho kinatarajia kukaa Aprili 29 mjini Dar es Salaam.