SERIKALI imepiga marufuku wahubiri wa dini na waganga wa jadi wanaojitangaza kuwa wana uwezo wa kutibu ugonjwa wa UKIMWI, kwani kufanya hivyo ni kuendelea kuchochea maambukizi ya ugonjwa huo ambao hadi sasa hauna tiba wala chanjo.
Akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Viti Maalumu, Lucy Mayenga (CCM) kuhusu watu wanaojitangaza kutibu UKIMWI wakati hauna tiba, Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Aisha Kigoda alisema watu hao ni wapotoshaji kuhusu hali halisi ya ugonjwa huo.
Alisema wananchi wawe makini na watu hao na wazingatie maagizo yanayotolewa na serikali kupitia wahudumu wake wa afya kuwa, UKIMWI hauna tiba yoyote zaidi ya dawa za kuongeza kinga ya mwili.
Akijibu swali la Msingi la Mbunge wa Viti Maalumu, Margareth Mkanga (CCM), aliyetaka kujua lini serikali itasitisha matumizi ya Kadi za Bluu zinazotumiwa na waathirika wa UKIMWI wakati wa kutibiwa kwani zinawanyanyapaa, Naibu Waziri huyo alisema kwa sasa serikali haina mpango wa kusitisha matumizi yake.
Alisema kuwa kadi hizo zinawasaidia wagonjwa wa UKIMWI kupatiwa tiba hata katika vituo ambavyo hawakuwa wakivitumia awali, kwani kwa kuonyesha vitambulisho hivyo, hutambuliwa na kupatiwa tiba.
Naibu waziri huyo alisema vitambulisho si sababu ya kuwepo kwa unyanyapaa, unatokana na uelewa wa jamii husika kuhusu ugonjwa huo kwani wapo wagonjwa wa kifua kikuu ambao nao pia hutibiwa kwa kutumia kadi za kijani.
Kwa upande wa wahudumu wa afya ambao wanaonyesha unyanyapaa kwa wagonjwa wa UKIMWI baada ya kuwaona wakitibiwa kwa kadi hizo za bluu, Naibu Waziri alisema serikali haitakuwa tayari kuwavumilia na kuahidi kuwachukulia hatua ikiwa ni pamoja na kuwafukuza kazi.