MISS India 1999, Yukta Mookhey, anatarajiwa kuwasili nchini leo kwa ndege ya Shirika la Qatar ambako atakuwa jaji katika shindano la kumsaka Miss Universe Tanzania, linalotarajiwa kufanyika keshokutwa katika Hoteli ya Movenpick, Dar es Salaam.
Mratibu wa shindano hilo, Mkurugenzi wa Kampuni ya Compass Communications, Maria Sarungi, alisema jana jijini Dar es Salaam kuwa, mara baada ya kuwasili, kwenye Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere majira ya saa 9:00 alasiri, Mookhey ataungana na kambi ya washiriki wa shindano hilo iliyoko Kunduchi Beach Resort.
Sarungi alisema kuwa mrembo huyo ambaye amepewa tiketi ya bure kwenda na kurudi na Shirika la Qatar Air, ataendesha maamuzi ya awali na kisha atawaeleza washiriki hao vigezo vinavyotakiwa katika kushiriki mashindano ya kimataifa ya urembo.
Miss India huyo ataungana na majaji wengine watano wazalendo ambao wameteuliwa kusimamia shindano hilo ambalo Miss Universe 2007 atashiriki shindano la kimataifa nchini Mexico.
Majaji wengine ni pamoja na Mkurugenzi wa Bodi ya Utalii, Peter Mwenguo, Dk. Ellen Otaru, David Nyombo na aliyekuwa Miss Earth Tanzania 2004, Sophia Byanaku.
Wareshiriki 25 wako kambini wakijinoa kwa ajili ya kinyang’anyiro cha Jumamosi ambacho kimedhaminiwa na kampuni mbalimbali zikiwamo Lowe Scanad na Roundtrip.