TAMASHA la kuhamasisha utalii wa ndani Tanzania, linatarajiwa kurindima Juni 2 kwenye viwanja vya Leaders, Kinondoni jijini Dar es Salaam.
Akizungumza jana kwenye Ukumbi wa Idara ya Habari (MAELEZO) jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Kamati ya Kuelimisha na Kukuza Utalii wa Ndani (KUK), Paschal Mabula, alisema lengo la kamati hiyo ni kuhamasisha jamii ya Watanzania kujenga utamaduni wa kutembelea vivutio vya kitalii vilivyoko nchini.
Mabula alisema kuwa, hivi sasa Watanzania wengi wana hisia za kuwa mtalii ni mtu kutoka nje ya nchi, hususan Ulaya.
Aliongeza kuwa, lengo la kuundwa kamati hiyo ni kuihamasisha jamii ya Kitanzania kujenga utamaduni wa kutalii kwani kufanya hivyo ni kujifunza na wala si anasa.
“Jamii haijaelimishwa vya kutosha kuhusu, utalii, hivyo tunawaasa kuwa waanze kutalii hivi sasa na gharama ni ndogo isiyozidi sh 2,000 kutembelea vivutio vya kitalii,” alisema.
Alisema Siku ya Utalii wa Ndani, itakuwa ikiadhimishwa kitaifa Juni 2, ya kila mwaka.
Mabula ambaye pia ni msanii wa kundi la Tanzania One Theatre (TOT), alisema katika tamasha la mwaka huu, kutakuwa na burudani ya muziki wa aina mbalimbali kutoka vikundi mbalimbali vya sanaa za maigizo, uchongaji na maonyesho ya kampuni zinazojishughulisha na utalii.
Naye mjumbe wa kamati hiyo, Mrisho Mpoto ‘Mjomba Mpoto’, alisema hivi sasa Watanzania lazima tujenge utamaduni wa kujivunia chetu.
Wajumbe wa KUK ni Mabula (Mwenyekiti), Ritha Paulsen (Mshauri), Mrisho Mpoto, Rose Ngonyani, Ally Yussuf, Hamza Kalala ‘Komandoo’ na Juma Tayari (Mratibu).