WAZIRI Mkuu mstaafu, Jaji Joseph Warioba, ameteuliwa na Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola, Don McKinnon, kuongoza timu maalumu ya waangalizi wa jumuiya hiyo, katika uchaguzi mkuu wa Nigeria.
Uchaguzi wa rais na bunge wa Nigeria, unatarajiwa kufanyika Aprili 21, mwaka huu.
Hii si mara ya kwanza kwa Jaji Warioba kuongoza timu ya waangalizi wa Jumuiya ya Madola katika chaguzi. Aliwahi kuongoza timu kama hiyo katika uchaguzi mkuu wa Malawi.
Aidha, ameshashiriki katika timu zilizoangalia chaguzi katika nchi za Zambia, Nigeria na Ethiopia.
McKinnon alisema timu hiyo inapelekwa kufuatia ombi lililotolewa na Serikali ya Nigeria na Tume Huru ya Uchaguzi ya nchi hiyo.
Alisema timu hiyo itakuwa na wajumbe tisa ambao ni watu maarufu, watakaosaidiwa na wajumbe saba wa sekretarieti ya jumuiya hiyo.
Pamoja na Jaji Warioba, wajumbe wa timu hiyo ni Joseph Biribonwa, ambaye ni Kamishna wa Tume ya Uchaguzi ya Uganda, Omar Jallow, Kaimu Katibu Mkuu na kiongozi wa Chama cha People’s Progressive cha Gambia na Dk. Noor Mohammad, Naibu Kamishna wa zamani wa Tume ya Uchaguzi ya India.
Pia wamo Robert Patterson, Afisa wa Uchaguzi wa zamani wa Columbia, Kareen Payne, mwakilishi wa kundi la vijana toka Antigua na Barbuda, Sheila Roseau naye kutoka Antigua na Barbuda, Nancy Tembo, mbunge toka Malawi na Martin Tete, Ofisa Mwandamizi wa uchaguzi kutoka Vanuatu