JUMLA ya watoto 100 wamezaliwa jijini Dar es Salaam katika mkesha wa Sikukuu ya Pasaka, iliyoadhimishwa jana duniani kote.
Kwa mujibu wa Ofisa Muuguzi wa Hospitali ya Temeke, Bahati Hamisi, jumla ya watoto 30 walizaliwa siku hiyo katika hospitali hiyo. Alisema kati yao, 15 ni wa kike na wa kiume ni 15 pia.
Ofisa huyo alisema kuwa watoto wote wamezaliwa salama na hali zao na za mama zao zinaendelea vizuri.
Katika Manispaa ya Ilala, jumla ya watoto 32 walizaliwa katika mkesha huo. Ofisa Muuguzi wa Hospitali ya Amana, Enjoy Kilangi, aliwaambia waandishi wa habari kuwa, kati ya watoto hao, 23 ni wa kike na tisa ni wa kiume.
Aidha, alifafanua kuwa akina mama wawili walijifungua mapacha. Mama mmoja alijifungua mapacha wote wa kike wakati mama mwingine alijifungua mtoto wa kiume na wa kike.
Taarifa iliyotolewa na muuguzi wa zamu wa Hospitali ya Mwananyamala, Grace Kombe, inaonyesha kuwa watoto 26 walizaliwa katika hospitali hiyo. Kati yao 13 ni wa kiume na 13 wengine walikuwa wa kike.
Katika Hospitali ya Taifa ya Muhumbili (MNH), jumla ya watoto 12 walizaliwa, kati ya hao, wa kike ni watano na wa kiume saba.