CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) wilayani hapa, mkoani Tabora, kimepanga kumvua madaraka, Diwani wa Kata ya Ndono, Musa Kayege, ambaye hivi karibuni alifikishwa mahakamani akikabiliwa na tuhuma za kumbaka mwanafunzi wa darasa la saba mwenye umri wa miaka 14.
Habari kutoka ndani ya CCM wilayani hapa, zinasema kuwa mipango ya kumvua diwani huyo madaraka, imeshaandaliwa. Habari hizo zimeongeza kuwa, kwa kulinda heshima ya chama hicho, diwani huyo atatakiwa kutangaza kujiuzulu.
Inaelezwa kwamba tuhuma zinazomkabili diwani huyo zimekishushia hadhi chama hicho.
Baadhi ya madiwani waliozungumza na gazeti hili lakini wakakataa majina yao kutajwa, walisema kuwa kitendo hicho kimewafedhehesha hata wao.
Walisema kuwa hivi sasa kila wanapopita mitaani wamekuwa wakizomewa huku wakiitwa madiwani wabakaji.
Naye Mwenyekiti wa halmashauri hiyo, Hamisi Bundala alisema tuhuma zinazomkabili diwani huyo ni nzito na zinawatia doa.
Alisema tangu mwenzao huyo afikishwe mahakamani, wamekuwa na wakati mgumu kwani baadhi ya viongozi wa kambi ya upinzani wamekuwa wakiwakejeli.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Uyui, Abdallah Kazwika, hakuwa na jibu la moja kwa moja kuhusu hatima ya diwani huyo mwenye tuhuma za ubakaji.
Alisema kwa sasa hawezi kusema chochote kwa kuwa suala hilo bado lipo katika vyombo vya sheria, lakini iwapo atatiwa hatiani, atafukuzwa uongozi.