SERIKALI imeanza kuendesha vikao vya mashauriano katika masuala ya utumishi wa umma kati ya Serikali ya Jamhuri wa Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.
Kikao cha kwanza cha mashauriano hayo kilifanyika jana Dar es Salaam chini ya uenyekiti wa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma), Hawa Ghasia.
Akifungua kikao hicho, Waziri Ghasia alisema wameamua kukutana ili kubadilishana mawazo kuhusu suala la utumishi wa umma katika Serikali ya Muungano.
“Utumishi bora, imara na wenye ufanisi ni muhimu kwa wananchi wa pande zote za Muungano. Kwa mantiki hiyo, hatuna budi kutafuta mbinu mbalimbali za kuimarisha utumishi wa umma wa serikali zote mbili.
“Kwa kufanya hivyo, tutaweza kutoa huduma nzuri kwa wananchi wetu na hatimaye kuleta maendeleo ya taifa letu,” alisema Ghasia.
Alisema kuwa kikao hicho kinatokana na azma ya serikali ya kuhakikisha kwamba wanalinda, wanadumisha, wanaendeleza na wanaimarisha muungano kwa faida ya pande zote mbili.
Alisema kwa upande wa utumishi wa umma, kikao hicho ni muhimu katika kuboresha na kuondoa kero za Muungano, hivyo akawataka washiriki kujadiliana kwa uwazi na moyo wa dhati huku wakiweka mbele maslahi ya taifa.