ASKARI wa Jeshi la Polisi wilayani Korogwe mwenye namba F. 5002, D/C Mohamed, amejeruhiwa vibaya baada ya kupigwa risasi sehemu za tumboni na mapajani katika harakati za kumkamata mmoja wa majambazi waliokuwa wameliteka basi la Kwekanga Line, lililokuwa likitokea wilayani Lushoto kuelekea jijini Tanga.
Majeruhi huyo amelazwa katika hospitali ya serikali Magunga, Wilaya ya Korogwe, mkoani Tanga.
Akizungumzia tukio hilo, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Tanga, Issaya Mngulu, ambaye alikuwa mmoja wa wapiganaji katika tafrani ya kurushiana risasi baina ya polisi na majambazi hao, alisema askari huyo alipigwa risasi na mmoja wa majambazi ambaye alikuwa akitumia bunduki aina ya gobori.
Alisema tukio hilo lilitokea juzi majira ya saa 11:00 alfajiri katika eneo la Mandui Mlola, Wilaya ya Lushoto, baada ya kundi la majambazi kuvamia basi hilo lenye namba za usajili T165 ADD, aina ya Fuso, lililokuwa likiendeshwa na Nassoro Ramadhani (31).
Mngulu alisema majambazi hayo yapatayo 10, yaliweka magogo barabani ili kuzuia gari hilo lisiweze kupita, na basi hilo liliposimama walilivamia na walifanikiwa kuwanyang’anya abiria waliokuwa zaidi ya 15 pamoja na dereva simu tano za mkononi zenye thamani ya sh 330,000 na vitu vingine vyenye thamani ya sh milioni 2.633.
Alisema katika msako aliouongoza yeye mwenyewe kwenye maeneo mbalimbali ya wilaya za Lushoto na Korogwe, walipambana na majambazi matano juzi majira ya saa 5:00 usiku.
Alisema katika mapambano hayo, walirushiana risasi na hivyo kufanikiwa kumkamata Omar Said (40), katika eneo la Mlingano wilayani Korogwe.
Aidha, alisema kutokana na upekuzi walioufanya nyumbani kwa mtu huyo aliyekamatwa, katika eneo la Makorora walikamata pia simu za selula tatu, fedha taslimu sh 213,000, pamoja na mifuko ya sulphate mitano iliyotobolewa kwa ajili ya kuficha sura.
Mngulu alisema imebainika kwamba mwenyeji mshiriki kwenye tukio hilo ni Said Athumani, maarufu kwa jina la Side, mkazi wa Mlola, wilayani Lushoto, ambaye inadaiwa kuwa aliwahi kufungwa kifungo cha nje baada ya kupatikana na hatia ya kosa la wizi, ambapo kufuatia tukio hilo la Machi 28 alitoroka kijijini kwake.