MKUU wa Jeshi la Polisi nchini (IGP), Said Mwema, amefanya mabadiliko ya ghafla katika vitengo viwili ndani ya jeshi hilo, kwa kile kilichoelezwa kuwa ni kuongeza ufanisi.
Habari zilizoifikia Tanzania Daima kutoka makao makuu ya jeshi hilo, zinaeleza kuwa IGP Mwema amefikia uamuzi huo ili kuleta mabadiliko ya kiutendaji katika vitengo hivyo.
Moja ya vitengo vilivyokumbwa na mabadiliko hayo ni Kikosi cha Usalama Barabarani, ambapo Mkuu wa Kikosi hicho nchini, Mselemu Mtulia, ameondolewa katika nafasi hiyo.
Taarifa zilizopatikana zinaonyesha kuwa Mselemu amehamishiwa makao makuu ya jeshi hilo. Hata hivyo, haikuweza kufahamika mara moja atapewa kazi gani.
Habari hizo zilieleza kuwa nafasi yake itachuliwa na James Kombe, ambaye kabla ya mabadiliko hayo alikuwa Mkuu wa Kikosi cha askari wa Kutuliza Ghasia (FFU).
“Sheria inampa mamlaka IGP kufanya mabadiliko wakati wowote anapoona kuna mahitaji au ulazima wa kufanya hivyo akijiridhisha. Kwa mfano, akiona malengo yanayotarajiwa hayakufikiwa,” alisema mmoja wa wapasha habari kutoka Makao Makuu ya Jeshi la Polisi ambaye hakupenda jina lake litajwe.
Alipotakiwa abainishe ni kwa nini mabadiliko hayo yamevigusa vitengo hivyo wiwili tu, alikataa kuingia kwa undani lakini alisema kuwa mtu anapewa kitengo kulingana na utendaji wake, lakini pia kuna vigezo vingine vingi vya kipolisi ikiwa ni pamoja na mapendekezo ya wakubwa.
Akizungumza na Tanzania Daima kwa njia ya simu jana, Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani anayehamishwa, Mselemu Mtulia, alikiri kuwapo kwa mabadiliko hayo.
“Ni kweli mabadiliko hayo yametokea, lakini ni ya kawaida kabisa, na tumeshakabidhiwa barua wiki moja iliyopita na leo (jana) ndiyo ninakwenda kuripoti makao makuu, lakini suala la makabidhiano ya ofisi za awali ni kesho,” alisema Kamanda Mtulia.