WATU 15 wakazi wa Kijiji cha Nungwi, wanashikiliwa na polisi kutokana na tuhuma za kumuua mzee mmoja baada ya kumtuhumu kuwa ni ‘popobawa’.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kaskazini Unguja, Mussa Ali Mussa alisema watu hao walikamatwa juzi kufuatia uchunguzi unaoendelea kufanyika katika kijiji hicho.
Alisema watu hao wanatarajiwa kufikishwa mahakamani kesho na watafunguliwa mashitaka ya mauaji.
Alisema watu hao walimuua mzee huyo juzi walipomuona akiendesha baiskeli akiwa amejifunga lubega huku akiwa amevaa bangili nyekundu katika mikono yake.
Kamanada huyo wa polisi alisema baadhi ya wananchi walianza kumfukuza katika eneo la Kivunge na baada ya kufika njia panda ya Kilindi na Kwenda walimkamata na kumpakia katika gari la abiria hadi kijijini Nungwi na kumpiga marungu na baadaye kumchoma moto pamoja na baiskeli yake.
Alisema mwili wa marehemu ulizikwa juzi na serikali ya kijiji kwa vile ulikuwa umeharibika vibaya na kwamba hadi sasa marehemu huyo hajatambuliwa jina lake wala sehemu anayotoka.
Kamanda huyo aliwataka wananchi kuacha kuchukua sheria mikononi, hasa kwa kuzingatia Zanzibar hakuna popobawa, isipokuwa ni imani potofu za kishirikina.
Kutokana na kamata kamata ya polisi, baadhi ya vijana wamelazimika kukimbia kijijini hapo tangu kutokea kwa tukio hilo.
Tukio hilo limekuja siku chache tangu Katibu wa Mufti wa Zanzibar, Sheikh Fadhili Soraga kuwataka masheikh wasome dua maalum kumuomba Mwenyezi Mungu kuwaepusha wananchi na kiumbe hicho kiitwacho popobawa.
Katika siku za hivi karibuni, Zanzibar imekumbwa na imani za kuwepo kiumbe popobawa ambapo watu 14 wamenusurika kuuawa baada ya kuzingirwa na wananchi waliowatuhumu ni popobawa.
Miongoni mwa matukio hayo ni lile lililotokea eneo la Kisima Mbaazi, Wilaya ya Mgharibi Unguja ambako watu wanane walikamatwa na wananchi na kutaka kushambuliwa na mawe walipokuwa wakicheza ngoma ya kijadi iitwayo Maswezi, ambayo ilikuwa imetolewa kibali na serikali.
Matukio mengine yalitokea Chumbuni, Jambiani, Kwamtipura na Bububu ambapo watu hao waliokoleewa na polisi.