VIONGOZI wa vyama vya upinzani visiwani hapa, wameshitushwa na kauli ya Rais Amani Abeid Karume, kuwa kiwango cha umasikini Zanzibar kimepungua kutoka asilimia 60 hadi 49 katika kipindi cha miaka mitano.
Waliyasema hayo kufuatia kauli aliyoitoa Rais Karume alipokuwa akizindua Mpango wa Kupunguza Umasikini Zanzibar (MKUZA) ambapo alisema hali hiyo imetokana na kuinuka kwa uchumi.
Rais Karume alisema uchumi wa Zanzibar umekua hadi kufikika asilimia 6.8 mwaka 2005 kutoka asilimia 5.6 ilivyokuwa mwaka 2002.
Katibu Mkuu wa TADEA, Juma Ali Khatib, alisema kwamba takwimu zilizotolewa na serikali ni sawa na kuwakejeli Wazanzibari, hasa wa kipato cha chini, ambao wanakabiliwa na ugumu wa maisha kutokana na kudorora kwa hali za maisha.
“Wataalamu wa uchumi Zanzibar wanadanganya wananchi kuhusu hali ya uchumi na umasikini, tunaomba rais atembelee vijijini ashuhudie hali za maisha ya wananchi,” alisema Khatib.
Alisema sekta ya biashara, inayotegemewa na watu wengi Zanzibar, imeanguka kwa kiasi kikubwa na kusababisha mzunguko wa fedha kuyumba.
Nae Naibu Mkurugenzi wa Haki za Binadamu na Mawasiliano ya Umma wa CUF, Salim Bimani, alisema chama chake kimeshitushwa na takwimu zilizotangazwa na serikali juu ya ukuaji wa uchumi wakati huduma za jamii zimeanguka.
Alisema kwamba, watu wanaomudu huduma za jamii pekee ni wale wenye uwezo, wakiwemo mawaziri, makatibu wakuu, wakurugenzi na baadhi ya wafanyabiashara.
“Zanzibar hivi sasa idadi ya ombaomba imeongezeka sana wakati zamani ilikuwa ni aibu, hata vijana wadogo wanaomba msaada mitaani,” alisema.
Alieleza kwamba sekta ya viwanda, ambayo ina mchango mkubwa katika ukuaji uchumi wa taifa lolote, imekufa hapa Zanzibar kutokana na sera mbaya na mipango mibovu ya maendeleo, ambapo bidhaa zote, ikiwemo za chakula zinaagizwa kutoka nje.
Alisema ili mipango Kukuza Uchumi na Kupunguza Umasikini (MKUZA) ufanikiwe, lazima kero za Muungano katika mfumo wa kodi na fedha zitatuliwe.
Bimani alisema kwamba tangu kuanza kwa mfumo wa kodi ya pamoja kati ya Tanzania Bara na Zanzibar, sekta ya biashara imeanguka na wananchi kukosa kazi, ikiwemo wachukuzi bandarini ambao hulazimika kulala chini ya miti muda mwingi kwa kukosa kazi.
Naibu Katibu Mkuu wa CHADEMA, Hamad Mussa Yussuf, alisema kwamba vigezo vinavyotumika katika kupima ukuaji uchumi Zanzibar vina utata mkubwa kwa vile hali inayotangazwa hailingani na halisi halisi ya vipato vya wananchi.
Alisema wakulima Zanzibar hivi sasa hawana tofauti na wakati wa mkoloni kwa vile uzalishaji wao umezidi kuanguka kutokana na kukosa zana za kisasa.
Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini wa UPDP, Haji Othman, alisema kwamba mwamko wa wananchi kujiajiri ni mkubwa, lakini wanarudishwa nyuma na watendaji serikalini, hasa Baraza la Manispaa.
Alisema nchi nyingi zinapiga hatua katika kuinua vipato vya wananchi kwa kuwaunga mkono wajasiriamali wanaojiajiri, lakini Zanzibar hakuna mkakati wa kuwasaidia wazalishaji wadogo wadogo.
Alisema hivi sasa sekta ya uwekezaji na biashara inakabiliwa na matatizo makubwa ya rushwa kutokana na kuzorota misingi ya utawala bora.