MAHABUSU walioko katika gereza la Keko, Dar es Salaam, ambao juzi walifikia muafaka wa kusitisha mgomo wao, wameipa serikali miezi mitatu kutekeleza madai yao, vinginevyo watajilipua kwa mabomu ya petroli.
Wakati wakitoa vitisho hivyo, wale walio katika gereza la Segerea, wamekataa kuitambua suluhu ambayo wenzao wa Keko walifikia na mawaziri wanne waliotembelea gereza lao juzi, kwa ajili ya kufikiwa muafaka baada ya kugoma kwa siku nne.
Mahabusu hao wa Keko, wamesema watatajitoa muhanga wa kujilipua kwa kutumia petroli wakati wakiwa ndani ya magari yanayowapeleka mahakamani, maarufu kama karandinga.
Hayo yalielezwa na mahabusu hao jana, wakati wakiwa katika viwanja vya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, pale mahabusu kutoka Segerea walipogoma kushuka kwenye gari kusikiliza kesi zao huku wenzao wa Keko wakishuka na kutoa masharti hayo mapya.
Mawaziri wanne, Mary Nagu (Katiba na Sheria), Bakari Mwapachu (Usalama wa raia), Joseph Mungai (Mambo ya Ndani) na Batilda Buriani (Ofisi ya Waziri Mkuu – Sera), juzi walilazimika kwenda Keko kusikiliza kwa undani madai ya mahabusu ambao kwa muda wa siku nne walikuwa wamegoma kushuka kwenye karandinga wakitaka upelelezi wa kesi zao uharakishwe.
Mahabusu hao waligoma baada ya kuharakishwa kwa kesi ya mauaji bila kukusudia, inayomkabili aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Ukiwaona Ditopile Mzuzuri, ambaye licha ya kudaiwa kutenda kosa hilo, Novemba mwaka jana, tayari ameshaachiwa kwa dhamana huku baadhi ya mahabusu hao wakisota kwa miaka kadhaa bila kesi zao kusikilizwa.
Wale wa kutoka Segerea, jana waligoma kushuka katika gari lao kwa madai kuwa wanataka kusikilizwa kama mahabusu wenzao wa gereza la Keko walivyosikilizwa na mawaziri, juzi.
Walisema hawakubaliani na kauli ya mawaziri hao kuwa mahabusu wa Keko waliwawakilisha katika mazungumzo hayo, kwa sababu matatizo na tabu wanazozipata wao, hazifanani na zile wanazozipata wenzao wa Keko.
“Sisi tuna malalamiko yetu na wa Keko wana yao, tunashangaa kuona mawaziri wakishindwa kutusikiliza na sisi… yaani sisi tuwakilishwe na wa Keko!… Ni vitu viwili tofauti na malalamiko si kesi peke yake, hata chakula,” alisikika mahabusu mmoja.
Kwa upande mwingine, mahabusu kutoka Keko, waliokuwa kwenye gari lenye namba STH 3058, walipokuwa wakiteremka, walisikika wakisema: “Licha ya kuzungumza na mawaziri juzi, lakini pia tumewapa miezi mitatu kutekeleza waliyotuahidi, kama hawatafanya hivyo tunaanza tena mgomo.”
“Hatutaki visingizio vya ucheleweshwaji wa kesi, tunajua kuwa sisi ni walalahoi tofauti na Ditopile na (Abdallah) Zombe (mkuu wa upelelezi wa zamani mkoani Dar es Salaam anayekabiliwa na kesi ya mauaji), lakini tunataka haki itendeke kwa wote,” alisema mmoja wao.
Kwa upande wao, mahabusu wa Segerea walitoa siku tano kwa mawaziri kuwatembelea na kama watashindwa kufanya hivyo, nao watajitoa muhanga kwa kujilipua au kugomea chakula ambacho hata hivyo walidai kuwa ni kibaya na hakifai kwa matumizi ya binadamu.
Baada ya mahabusu hao kugoma kushuka, gari liliondoka saa 4:15 na kuwarudisha gerezani.
Wakati wakiondolewa mahakamani hapo, walitoa mabango yaliyokuwa yameandikwa madai yao ikiwa ni pamoja na kutaka kuonana na Waziri Mkuu, Edward Lowassa, Dk. Nagu, Mungai na Mwapachu ili wazungumze nao.
Mbali na ujumbe huo, walikuwa wanamtaka Mwendesha Mashitaka Mkuu wa mahakama za Kisutu na Temeke wajiuzulu kwa madai kuwa mahakama hizo zinanuka kwa rushwa.