KWA mara ya kwanza serikali imekiri hadharani kuwa ule msemo kwamba watu wote ni sawa mbele ya sheria, ni danganya toto.
Serikali pia imeonyesha bila kificho kuwa msemo mwingine, sheria ni msumemo, hukata mbele na nyuma, ambao hutumiwa kuonyesha kuwa watu wote wana haki sawa mbele ya sheria, kuwa ni uongo.
Sasa serikali imewaonyesha wananchi kuwa mtu mwenye dhamana fulani katika jamaii, iwe ya kupewa au kujipa, ana haki sana mbele ya sheria kuliko mnyonge.
Na wanapoamua hao wenye kushika mamlaka wanaweza kumnyonga mnyonge huyo bila kujali kwamba naye ni binadamu, ingawa hali yake ni dhalili.
Nimeanza na msimamo huo kutokana na kauli zilizotolewa wiki hii na Waziri wa Usalama wa Raia, Bakari Mwapachu, na Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Kamishna Alfred Tibaigana, wakitetea mambo kadhaa yaliyotokea yakihusiana na kesi ya aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Ukiwaona Ramadhan Ditopile Mzuzuri.
Katika kauli yake, Mwapachu aliwaeleza waandishi wa habari kuwa suala la kesi ya mtu fulani kwenda haraka si jambo la ajabu na halistahili kuleta manung’uniko katika jamii hata kama kuna watu wamesota rumande kwa miaka mingi.
Mwapachu alisema kuwa Ditopile ana bahati kwamba ana fedha nyingi kiasi cha kuweza kuajiri mawakili wazuri ambao wameisimamia kesi yake na kuhakikisha kuwa anaachiwa kwa dhamana muda mfupi baada ya mashitaka yake kufikishwa mahakamani.
Inaweza kuonekana kuwa miezi minne ambayo Ditopile amesota rumande ni muda mrefu sana, lakini ukiulinganisha muda huo na miaka zaidi ya 10 ambayo baadhi ya mahabusu wamekuwa wakisubiri kukamilika kwa kesi zao ili upelelezi uanze, miezi hiyo minne inaonekana kama tone la maji baharini.
Kwamba, uwezo wa kifedha ni moja kati ya vigezo ambavyo vinaweza kumsaidia mtu apate haki, ndilo suala ambalo limenishtua sana, hasa lilipotamkwa na mtu mwenye dhamana ya Mwapachu.
Haiyumkiniki kwa waziri katika serikali iliyochaguliwa kwa zaidi ya asilimia 80 ya Watanzania, ambao wengi wao ni waamka hoi (baada ya kulala hoi), leo kuwageuka na kuwalaumu wanaolalamika kwa kusota rumande, kuwa kutokuwa kwao na fedha ndilo tatizo linalokwamisha haki zao.
Kitu ambacho wengi tulikuwa tunakiamini ni kuwa mfumo wetu wa sheria haubagui mwenye fedha au asiye nazo, mrefu au mfupi, Mmakonde au Mndengereko, mkuu wa mkoa au tarishi n.k.
Huo ndio mfumo tuliojijengea kwa wananchi na kuwapa imani na vyombo vinavyosimamia sheria na kutoa haki kama polisi na mahakama.
Lakini Mwapachu ametufumbua macho kwa kutueleza kuwa ukiwa na fedha, hali inakuwa tofauti kidogo kwani unaonekana kuwa ni mwenye haki sana kuliko mtu mwingine wa kawaida.
Haishangazi basi, wapo baadhi ya watu ambao walipatwa matatizo ya kisheria, lakini kesi au mashauri yao yakachukua muda mfupi sana kushughulikiwa na kukamilishwa.
Na wapo Watanzania wengine ambao kwa miaka mingi sana wamekuwa wanasota rumande wakisubiri kukamilika kwa taratibu ili kesi zao zianze kusikilizwa.
Kamishna Tibaigana naye kaja na yake. Akihalalisha jinsi polisi walivyomlinda Ditopile, anasema waliwajibika kufanya hivyo kwa ajili ya usalama wake.
Sina ugomvi na ukweli kwamba polisi wanatakiwa kuhakikisha usalama wa watuhumiwa wawapo mikononi mwao.
Lakini kwa jinsi Ditopile alivyolindwa, mpaka kufikia hatua ya askari hao kuwasaidia ndugu zake kupiga waandishi wa habari, inatia shaka kwamba polisi walikuwa wanatimiza wajibu wao wa kuhakikisha Ditopile anakuwa salama.
Hivi pale Mahakama Kuu, polisi walipopiga waandishi, Tibaigana anataka kutuambia kuwa polisi hao walibaini kuwa waandishi wana lengo la kumdhuru Ditopile?
Au Polisi walipoamua kumpandisha cheo Ditopile na kuwa jaji na kumpitisha kwenye mlango wanaopaswa kupitia majaji, kulikuwa na jambo gani ambalo lingehatarisha usalama wa mtuhumiwa huyo iwapo angepitishwa kwenye mlango wa kawaida wanaopitia watuhumiwa wengine na polisi wakashindwa kuhakikisha usalama wake?
Hata kama ni kweli kuwa Ditopile angedhuriwa na mahabusu wengine iwapo angesafirishwa kwenye gari moja nao, Kamishna Tibaigana na wenzake wanapaswa kujiuliza ni kwa sababu gani mahabusu hao wangemdhuru?
Mbona kila siku wanasafirishwa wenyewe kuja mahakamni na kurejeshwa rumande lakini hatujasikia kwamba wamemdhuru mwenzao? Iweje wawe na nia ya kumdhuru Ditopile tu? Au ulikuwa ni woga wa Tibaigana?
Uchunguzi juu ya hilo ungemwezesha Tibaigana na kundi lake kubaini moja ya sababu zinazosababisha malalamiko kutoka kwa mahabusu wengi ambao hivi sasa wapo kwenye mgomo wakidai kuonana na Waziri Mkuu, Edward Lowassa.