WATU 12 wamefariki dunia na wengine zaidi ya 30 kujeruhiwa, baadhi yao vibaya, baada ya basi walilokuwa wakisafiria kugongana uso kwa uso na lori la mizigo aina ya Fuso, katika Barabara ya Morogoro-Dodoma, eneo la Mkundi, katika Manispaa ya Morogoro. Ajali hiyo ilitokea jana majira ya saa 7 mchana.
Majeruhi mmoja aliyejitambulisha kwa jina moja la Diana, alisema kuwa ajali hiyo ilitokea wakati wao wakiwa kwenye gari lenye jina la Mwandike Express lenye namba za usajili T 369 AAR, wakitokea jijini Dar es Salaam, kuelekea Mvumi mkoani Dodoma.
Alisema kuwa ajali hiyo ilitokea baada ya gari lao kugongana uso kwa uso na lori hilo la mizigo, lenye namba za usajili T 803 ADR, lililokuwa likija mbele yao huku likiyumbayumba barabarani.
Majeruhi huyo alisema kuwa waliofikishwa hospitalini hapo ni majeruhi wachache tu kwani wengi zaidi wamefunikwa na Fuso hilo lililopinduka baada ya kugongana na basi.
Katika ajali hiyo, watu wawili walifariki dunia mara baada ya kufikishwa katika Hospitali ya Mkoa wa Morogoro. Wametambuliwa kuwa ni Rosemary Charles (4), mkazi wa Ukonga jijini Dar es Salaam na Saidi Vulambika anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka 36-37.
Aidha, majina ya marehemu wengine hayajaweza kutambuliwa.
Kwa mujibu wa watu walioshuhudia ajali hiyo, chanzo chake inadaiwa kuwa ni dereva wa lori hilo kujaribu kulipita basi.
Waliojeruhiwa katika ajali hiyo ni zaidi ya 33 ambapo baadhi yao ni Felista Chilumati (18), mkazi wa Dodoma, Abdallah Shalude (36), Damasi Chilunduka (22) kutoka Mvumi, Oscar Chilundulu (miezi minane) naye mkazi wa Mvumi, Daniel Msilimka (46) mkazi wa Dodoma, Steven Edger (25), Magubike, Jackson Mwanja (42) na Anjelina Musa (9) wote wakazi wa Dar es Salaam.
Wengine ni Daniel Kisiluka, Ashura Bakari, Asheri Mgusha, Francis Mlela, Subira Sanjila, Julius Msenga mkazi wa Kibaigwa, Azalia Akisa, Janeth Makha, Neema Kusilimuka, Mary Msemakweli (15), Nodya Obedi (48) wa Dar es Salaam, Eva Mabwe (35) naye mkazi wa Dar es Salaam, Christina (3), Luben Kefa (7) wa Dar es Salaam, Pendo Muyangale (18), Jailos Masamla (39) wa Dar es Salaam, Ester William (5) wa Dar es Salaam.
Aidha, majeruhi hao wamelazwa katika Hospitali ya Mkoa wa Morogoro na baadhi yao hali zao ni mbaya sana. Miili ya marehemu imehifadhiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti hospitalini hapo.
Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai mkoani hapa, Ahmed Msangi, alithibitisha kutokea kwa ajali hiyo. Hata hivyo, hakuwa tayari kueleza chanzo cha ajali hiyo kwa madai kuwa polisi bado wanachunguza.