MKAZI wa kijiji cha Nkundi wilayani Nkasi, Lucas Simba (54) anashikiliwa na polisi kwa tuhuma ya kumuua kwa kumchoma kisu mke wake na kumchinja mtoto wake wa kambo.
Kaimu Kamanda wa Polisi mkoa wa Rukwa, Germanus Mponguliana, aliwataja waliouawa kuwa ni Daudi Mapunda (mwenye umri wa miezi minne), ambaye ni mtoto wa kambo wa mtuhumiwa, na mkewe, Pili Ulungu (40) ambaye alimuua kwa kumchoma kisu tumboni hadi kufa.
Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari jana na Kaimu Kamanda ilieleza kuwa tukio hilo lilitokea hivi karibuni usiku kwa kinachodaiwa kuwa ni ugomvi wa kimapenzi.
Ilielezwa kuwa Simba kabla hajafanya mauaji hayo alikuwa na ugomvi na mkewe, baada ya kurejea nyumbani na kuanza kumpiga mke wake, akachukua kisu kilichokuwa mezani na kumchoma kwenye titi la kushoto, hali iliyosababisha kutokwa na damu nyingi na kufariki dunia.
Mtoto katika mazingira hayo alianza kulia kwa kupiga kelele, hatua iliyomfanya mtuhumiwa kumkamata, akampiga kofi, na baada ya kuanguka alimwinua, na kuanza kumchinja kwa kutumia kisu ambapo alitenganisha kichwa na kiwiliwili.
Habari zaidi zinadai kuwa Simba wakati akimalizia kumchinja mtoto majirani walitokea na akatimua mbio.
Majirani walimkimbiza, akaingia kichakani, akazingirwa ndipo alipokurupuka na kumrukia mmoja wao na kumchoma kwa kisu tumboni na kumwacha utumbo ukining'inia nje.
Mponguliana alimtaja aliyjeruhiwa kwa kuchomwa kisu tumboni kuwa ni Joseph Lupia (20), mkazi wa kijiji hicho, ambaye amelazwa katika wodi ya wagonjwa mahututi kwenye hospitali ya serikali ya mkoa wa Rukwa.
Kuona hivyo wanakijiji walitumia nguvu za ziada na kufanikiwa kumkamata Simba, ambapo inaelezwa kuwa kwa kutumia kisu kile kile alichofanyia mauaji walimkata sikio la kulia na kumjeruhi mikono yote miwili, na baadaye kumpeleka kituo cha polisi.
Simba anatarajiwa kufikishwa mahakamani wakati wowote kuanzia sasa kujibu tuhuma zinazomkabili.